Pages

KAPIPI TV

Saturday, November 1, 2014

KIKAO CHA BARAZA KUU LA WAFANYAKAZI WA SHIRIKA LA NYUMBA(NHC)CHAFANYIKA JIJINI TANGA


Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu, akimsindikiza Mgeni Rasmi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo Japan Kidata kuelekea kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, katika Ufunguzi Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo.
Katibu wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa, Mecktilda Mihayo akijadiliana jambo na Veronica Mtemi na Katibu Msaidizi wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa, Adolph Kasegenya wakati wakisubiri kumpokea Mgeni Rasmi, Katibu Mkuu wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo Kidata.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu na Mgeni Rasmi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo Japan Kidata wakisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Luteni Chiku Gallawa kabla ya kuelekea kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, katika Ufunguzi Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo.
Mgeni Rasmi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo Japan Kidata akikaribishwa na Katibu wa Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa, Mecktilda Mihayo kuelekea kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, katika Ufunguzi Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo. Kulia kwake ni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza hilo.
Mgeni Rasmi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo Japan Kidata akikaribishwa na Mkurugenzi wa Usimamizi Miliki wa NHC, Hamad Abdallah huku Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano kwa Umma na Huduma kwa Jamii (Katikati), Susan Omari kuelekea kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, katika Ufunguzi Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo.
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu akimuongoza Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo JapanKidata kuingia kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, katika Ufunguzi Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo.
Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Sheria wa NHC, Martin Mdoe akijadiliana jambo na Meneja Madeni wa Shirika la Nyumba la Taifa, Joseph Mwanasenga wakati wakisubiri Mgeni rasmi.
 Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) wakiimba wimbo wa ‘Solidarity Forever’ ikiwa ni ishara ya kuhimiza ushirikiano miongoni mwa wafanyakazi wakati Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo Japan Kidata walipokuwa wakiingia kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, katika Ufunguzi Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo.
 Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Alphayo Japan Kidata wakiwa wamewasili kwenye meza yao.
 Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu akiwahutubia wajumbe wa Kikao Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).
Sehemu ya Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) wakifuatilia Ufunguzi wa Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo kinachofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, 
 Meneja wa Manunuzi wa NHC, Michael Chilongani, Afisa Mauzo wa NHC Gibson Mwaigomole wakifuatilia Ufunguzi wa Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo kinachofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, 
Meneja wa Huduma kwa Jamii, Muungano Saguya na Pastory Pauline wakifuatilia Ufunguzi wa Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo kinachofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, 
Meneja wa Huduma kwa Jamii, Muungano Saguya na Emmanuel Abdallah wakifuatilia Ufunguzi wa Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo kinachofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, 
 Sehemu ya Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) wakifuatilia Ufunguzi wa Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo kinachofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, 
Sehemu ya Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) wakifuatilia Ufunguzi wa Kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika hilo leo kinachofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Hoteli ya Tanga Beach Resort Tanga, 
Picha ya pamoja ya Wajumbe wa kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa kinachofanyika leo hoteli ya Tanga Beacha Resort, Tanga.
Picha ya pamoja ya Wajumbe wa kikao cha Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Shirika la Nyumba la Taifa kinachofanyika leo hoteli ya Tanga Beacha Resort, Tanga.
 
&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&
 
HOTUBA YA KATIBU
MKUU, WIZARA YA Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, BW. ALFAYO JAPAN KIDATA, kwenye
ufunguzi wa kikao cha baraza kuu la wafanyakazi, mjini TANGA tarehe 1 NOVEMBA,
2014
 
Ndugu Nehemia Kyando Mchechu, Mkurugenzi
Mkuu wa Shirika na Mwenyekiti wa Baraza Kuu la Wafanyakazi,
Ndugu Wakurugenzi,
Ndugu Wajumbe wa Baraza,
Wageni Waalikwa,
Wanahabari,
Mabibi na Mabwana,
 
Awali ya yote,
napenda nianze kwa kuishukuru Menejimenti ya Shirika, kwa kunipa heshima ya
kuja kuwa Mgeni Rasmi kwenye ufunguzi wa Baraza hili. Nawashukuru sana.
 
Nawashukuru kwa
sababu tukio hili la leo limenipa fursa ya kukutana na watendaji wakuu na
wawakilishi wa wafanyakazi kutoka Mikoa yote ya Shirika kwa mara ya kwanza
tangu niteuliwe kuwa Katibu Mkuu wa Wizara yetu. Hivyo, ni fursa kwangu kuweza
kufikisha ujumbe kwa wafanyakazi na umma juu ya Shirika letu.
 
Ndugu Mwenyekiti, nichukue fursa hii pia kuwapa wajumbe wote pole kwa safari ya masafa
marefu mpaka kufika hapa Tanga. Naamini kuwa uchovu wenu umemalizwa na hali nzuri
ya hewa ya Jiji hili la Tanga pamoja na ukarimu wa Wana-Tanga ukiambatana na
usemi wao “waja leo, warudi leo”. Bila shaka hamtarudi leo kama usemi huu
unavyosema maana Tanga kuna vivutio vingi vya kufurahia ikiwemo bandari kongwe,
mapango ya Amboni na fukwe zenye mandhari nzuri. Msije mkaondoka Tanga bila
kula ugali wa mhogo maarufu kama BADA, kuku wa mchemsho na mchunga.
 
Ndugu Mwenyekiti, nimefahamishwa kuwa Baraza hili limetanguliwa na mikutano ya Mameneja
wa Mikoa na mapitio ya Mpango Mkakati wenu kwa nia ya kutengeneza Mpango
Mkakati  mwingine kwa miaka kumi ijayo. Sisi
katika Wizara tumefarijika sana kuona kuwa Menejimenti ya Shirika inatambua
umuhimu wa kuwapatia viongozi wake wa Mikoa ujuzi katika uongozi kwani uongozi
bora na makini huchangia sana katika kuleta tija. Aidha, niwapongeze kwa
kutengeneza Mpango Mkakati mzuri wa miaka mitano ambao unamalizika mwaka ujao.
Kila mmoja na hata Taifa letu linatambua kuwa Mpango Mkakati wenu umeleta tija
kubwa na mmeweza kuutekeleza kwa mafanikio makubwa sana. Hongereni sana.
Ndugu Mwenyekiti, nimeelezwa pia kuwa ajenda za kikao cha Baraza hili zitahusu kujadili
mambo ya utendaji kwa ujumla yanayohusu maendeleo ya Shirika mliyojiwekea
kwenye Mpango Mkakati wa miaka mitano. Aidha, nimeelezwa kuwa kikao chenu
kitapitia mizania ya hesabu za Shirika kwa mwaka 2014/2015, pamoja na kujadili
taarifa za utekelezaji wa mambo mliyojiwekea katika Mpango Mkakati wenu. Naupongeza
sana utaratibu huu maana unaleta mezani kwa pamoja utekelezaji wa majukumu ya
kazi na kuainisha changamoto zilizokuwepo kwa nia ya kuzipatia ufumbuzi uliyo
makini zaidi.
 
Ndugu Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe, sina haja ya kusisitiza umuhimu wa ajenda zote hizi
zilizoko mbele yenu, kwani naamini wajumbe wote wa Baraza hili mnatambua
umuhimu wake. Hivyo, ni matarajio yangu kuwa ajenda hizi, ambazo zinagusa uhai na
maendeleo ya Shirika letu, mtazijadili kwa kina ili hatimaye muweze kutoka na
maazimio makini yatakayoliwezesha Shirika hili kuongeza tija na kukidhi
matarajiyo ya umma wa watanzania, ambayo kwa sasa yako juu sana kutokana na
imani mliyowajengea.
 
Ndugu Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe, napenda pia kuchukua fursa hii kuwapongeza wafanyakazi
wa Shirika kwa kutenda kazi zenu kwa ufanisi mkubwa. Inafurahisha kuona kuwa
hivi sasa mmejipanga vilivyo kupanua shughuli za ujenzi wa nyumba hususan za
gharama nafuu katika mikoa mbalimbali hapa nchini. Kipekee niwapongeze kwa
kurejesha utaratibu aliouanzisha Baba wa Taifa wa kuanza kwa kasi ujenzi wa
nyumba za gharama nafuu katika miji mbalimbali ya Halmashauri za Miji na Wilaya
nchini. Nafahamu kuwa hivi sasa mmeshaifikia mikoa 19 na mnayo matumaini
makubwa ya kufikia mikoa yote kufikia Desemba mwaka huu. Utaratibu huu unaolenga
kuwawezesha wananchi wa kipato cha kati na chini kumiliki nyumba, umepongezwa
sana na Serikali Kuu na viongozi mbalimbali wakiwemo Waheshimiwa Wabunge. Hivyo,
mnayo dhima na jukumu kubwa la kuusimamia mpango huu ili ndoto hiyo ya kuwawezesha
watu wengi kumiliki nyumba iweze kutimizwa. Bila shaka mkifikia lengo hilo,
mtakuwa mmeweka msingi mkubwa wa kukumbukwa katika Taifa letu na vizazi vijavyo
kama tunavyomkumbuka Baba wa Taifa wa kueneza ujenzi wa nyumba za gharama nafuu
katika miji mingi baada ya Uhuru wa Taifa letu.
Ili kuzifanya nyumba
hizi mnazojenga kuwa nafuu, narudia kusisitiza agizo alilolitoa Mheshimiwa Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kuwa Halmashauri
za Miji na Wilaya zilipatie Shirika la Nyumba na waendelezaji wengine wa Miliki
maeneo ya kujenga nyumba hizo bila kuhitaji fidia kubwa. Aidha, Wizara yangu
itaendelea kuzishawishi taasisi zinazotoa huduma za msingi za makazi kama vile
umeme, maji na barabara kutimiza wajibu wao kwa kupeleka huduma hizo katika
maeneo ya ujenzi wa nyumba. Kwa kuwa hili pia ni agizo la Mheshimiwa Waziri
Mkuu alilolitoa wakati akizindua ujenzi wa nyumba za NHC, Medeli, Dodoma tarehe
13/8/2011. Nina imani kuwa taasisi zote husika zitatekeleza jambo hili. Napenda
kulipongeza Shirika la umeme Tanzania kwa kuanza kupeleka huduma zake katika
maeneo mapya ya ujenzi wa nyumba. Niwahakikishie kuwa Wizara yangu itaendelea
kufuatilia kwa karibu jambo hili.
 
Ndugu Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe, nafarijika pia kuwapongeza kwa dhati kwa kuboresha
huduma zenu mnazowapa watanzania. Hivi sasa unapopita katika miji mingi hapa
nchini unashuhudia nyumba nyingi za Shirika zikipendeza baada ya kufanyiwa
matengenezo makubwa. Vilevile, kipekee niwapongeze kwa kuweza kukusanya kodi na
malimbikizo yaliyokuwepo huko nyuma bila woga jambo ambalo limewezesha kujenga
nidhamu kwa wapangaji wenu ya kulipa kodi. Hivi sasa Wizara yangu haipokei
malalamiko mengi kutoka kwa wapangaji na wafanyakazi wenu kutokana na
Menejimenti kujitahidi kuondoa kero mbalimbali kwa kuhakikisha kuwa kila
mfanyakazi anatenda kazi zake kwa uwazi, uadilifu na weledi wa hali ya juu. Mambo
hayo yote kwa ujumla yamewaongezea heshima kubwa na kujenga taswira nzuri ya
Shirika katika jamii ya watanzania. Hongereni sana na endeleeni kutenda kazi
zenu kwa juhudi na maarifa mkitambua umuhimu mkubwa wa sekta ya nyumba
tuliyowapa dhamana ya kuisimamia.
Ndugu Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe, nichukue pia fursa hii kuwapongeza kwa dhati kwa uamuzi
wenu wa kizalendo mlioufanya na kuutekeleza wa kuwapatia vijana mashine za
kufyatulia matofali katika Halmashauri zote za Wilaya Tanzania. Uamuzi huu
makini na ulioutukuka umesaidia juhudi za serikali za kuondoa umaskini miongoni
mwa vijana kwa kuwapatia ajira vijana hao. Kama mnavyofahamu vijana wasipokuwa
na kazi ya kufanya hujiingiza katika uhalifu na kuhatarisha amani ya nchi. Tumefurahi
kuona kuwa hivi sasa mmeshirikiana na Mamlaka ya Ufundi Stadi nchini (VETA)
kuwpa vijana mafunzo ya namna ya kutumia mashine hizo kutengenezea matofali.
Teknolojia hii mliyoibuni ya kutengeneza matofali kwa kutumia mashine hizi inatumia
sementi kidogo kuzalisha matofali na kwa hiyo  haiharibu mazingira kwa kuwa hakuna miti
inayokatwa ili kuchomea matofali. Tunaupongeza utaratibu huu ambao umetoa ajira
kwa vijana na tunataraji kuwa mtaongeza ushirikiano huo na VETA kwenye maeneo
mengine ya ujenzi kama upigaji wa rangi, useremala, umeme, uwekaji marumaru na
bomba ili kuwapa vijana wengi zaidi ujuzi na ajira. Endeleeni na utaratibu huu
ambao hata Rais wetu Mheshimiwa Dk. Jakaya Kikwete ameupongeza sana wakati
akihutubia Taifa katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani ambayo
kitaifa yalifanyika Jijini Mbeya. Hivyo,nichukue fursa hii kuwasihi Mameneja wa
Shirika wa Mikoa kusimamia utekelezaji wa program hii ili iweze kuleta tija
iliyokusudiwa na Shirika na Serikali yetu.
Ndugu Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe, kama mnavyofahamu hapa nchini kuna uhaba mkubwa wa
nyumba unaokadiriwa kufikia nyumba milioni tatu. Pamoja na juhudi na ubunifu
mbalimbali mliyoufanya uliosaidia kuongeza kasi ya ujenzi wa nyumba za kada
zote, Serikali yenu inaamini kuwa mkiongeza kasi zaidi katika ujenzi wa nyumba,
licha ya kuwa mtakuwa mmetekeleza ilani ya uchaguzi ya chama tawala, mtakuwa
pia mmeisaidia Serikali katika juhudi zake za kuondoa umaskini nchini.
Ndugu
Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe, nawaomba muendelee na juhudi hizo
mlizozionyesha ili
hatimaye chombo hiki muhimu cha serikali kiweze kukidhi matarajio ya
umma wa Watanzania.  Kama mlivyokwishasikia, upande wa serikali
tunajitahidi
kuboresha sera ya nyumba na sheria mbalimbali ili kufanya sekta ya
nyumba hapa
nchini iweze kuchangia kikamilifu pato la Taifa.
Ndugu Mwenyekiti na Ndugu wajumbe, Serikali inafahamu kuwa zipo changamoto nyingi
zinazoikabili sekta ya nyumba ikiwemo gharama kubwa  ya vifaa vya ujenzi na upatikanaji wa mikopo
ya nyumba ya muda mrefu yenye riba nafuu.  Napenda kuwahakikishia kuwa Serikali
inazifanyia kazi changamoto hizo ili kuifanya sekta ya nyumba iwe na mchango
mkubwa wa uchumi na jamii kwa ujumla. Hata hivyo, nyie kama wataalamu wa
ujenzi, mnapaswa mara kwa mara, na hata kupitia kikao muhimu kama hiki, kuishauri
serikali yenu namna bora ya kuwezesha wananchi kujengewa au kujenga nyumba za
gharama nafuu, kama mkakati mmojawapo wa kuondoa umaskini kwa wananchi wetu.
Ndugu Mwenyekiti na Ndugu Wajumbe, naelewa kuwa kodi ya nyumba kwa muda mrefu sasa
imekuwa ndiyo uti wa mgongo wa mapato ya Shirika. Pamoja na kusisitiza umuhimu
wa kuikusanya kodi hiyo, napenda vile vile nitoe wito kwa wapangaji wote nchini
wanaodaiwa kodi na malimbikizo wajitahidi kulipa kodi hiyo ili Shirika liweze
kujenga nyumba mpya na kutengeneza nyumba zilizopo kama ilivyopangwa. Wajibu
huo wa kulipa kodi umo ndani ya mikataba yao ya upangaji. Wapangaji wafahamu kuwa
kodi ndiyo inayotumika kutoa huduma bora kwao na kwa wananchi wengine. Wafahamu
kuwa nyumba wanazopanga kimsingi ni mali ya watanzania wote na kwamba wao
wamebahatika tu kupata fursa hiyo adimu ambayo kimsingi wanapaswa kuienzi kwa
kulipa kodi kwa wakati. Aidha, wafahamu kuwa kodi ya nyumba za Shirika iko
chini ukilinganisha na wamiliki wengine wa nyumba nchini. Ni vema sasa Shirika
likarekebisha viwango vya kodi ya nyumba zenu ili viendane na hali halisi ya
sasa, inagawa haitafikia viwango vinavyotozwa na wamiliki wengine.
Ndugu Mwenyekiti na Ndugu wajumbe, yapo mengi ya kuongea. Hata hivyo, nisingependa kuwachosha
kabla ya kuanza kazi kubwa inayowasubiri. Hivyo, naomba niishie hapa kwa
kuwashukuru tena kwa kunipa heshima ya kuzungumza nanyi kupitia Baraza hili. Ni
matumaini yangu kuwa maazimio mtakayopitisha hapa mtakwenda kuyatekeleza kwa vitendo
na kwa uadilifu mkubwa, ili kuliwezesha Shirika letu kutoa huduma za makazi
zilizo bora kwa wananchi.
 
Baada ya kusema hayo, Ndugu Mwenyekiti, sasa napenda kutamka kuwa Kikao cha Baraza lenu la
Wafanyakazi kimefunguliwa rasmi. Nawatakia kikao chema na ahsanteni kwa
kunisikiliza.

No comments: