Spika
wa Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Dkt. Magret Zziwa (wa
pili kulia) akipewa maelezo na Mtendaji Mkuu wa kampuni ya TICS Paul
Wallace namna kampuni yake inavyofanyakazi ya kupakua na kupakia mizigo
katika bandari ya Dar es salaam wakati wa ziara ya Wabunge wa bunge hilo
walipotembelea ofisi za Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) jana jijini
Dar es salaam.
Picha na Eleuteri Mangi-MAELEZO)
…………………………………………………
Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
29/08/2014
Jumuiya ya Afrika Mashariki iko
makini katika kutekeleza majukumu yake na iko karibu na watu wake kwa
kuwahudumia kupitia nchi washirika.
Kauli hiyo imetolewa na Spika wa
Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Dkt. Magret Zziwa wakati wa
ziara yake alipotembelea ofisi za Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA)
pamoja na wabunge wa bunge hilo jana jijini Dar es salaam.
Spika Dkt. Zziwa alibainisha kuwa
lengo la ziara ya wabunge hao ni kujionea shughuli mbalimbali
zinazofanywa na TPA na Bandari ya Dar es salaam kwa ujumla katika
kuhudumia nchi washirka kiuchumi na kujiamii.
“Ni muhimu kuifanya Jumuiya kuwa
imara zaidi kiuchumi na kijamii ili kuwahudumia watu wetu kwa umahiri na
umakini mkubwa katika mahitaji yao” alisema Spika Dkt. Zziwa.
Wabunge hao walitembelea maeneo
mbalimbali bandarini hapo na kujionea shughuli zinazofanywa ikiwa ni
pamoja na kupakia na kupakua mizigo inapoingia au kutoka ili
kusafirishwa kwenda nchi husika.
Spika Dkt. Zziwa alisisitiza kuwa
wananchi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wanahitaji kuona jumuiya yao
inavyowajali na kuwahudumia wanapotekeleza majukumu yao ikizingatiwa
kuwa kwa sasa hakutakuwa na urasimu wa kusafirisha mizigo kutoka nchi
moja kenda nyingine kwa kukaguliwa mara mbili ambapo kwa sasa utaratibu
wa Himaya Moja ya Forodha umeanza kutekelezwa kwa mafanikio makubwa.
Akionesha umuhimu wa uchukuzi na
usafirishaji wa mizigo kati ya nchi washirika, Naibu Waziri wa Wizara ya
Ushirikiano ya Afrika Mashariki, Dkt. Abdala Juma Abdulla Saadalla
amefananisha bandari, reli na barabara katika nchi kuwa ni sawa na “moyo
na mishipa ya damu” ambapo amebainisha kuwa Serikali ya Tanzania
inaendelea kuboresha reli zilizopo ili ziweze kutoa huduma kwa wakati.
“Tayari Serikali kupitia wataalamu
wake wa ndani imeboresha vichwa vya treni nane hadi sasa ambapo
vinatarajiwa kuanza kutumika Januari mwakani pamoja na makasha” alisema
Naibu Waziri Saadalla.
Kwa upange wake Meneja wa Bandari
ya Da es salaam Awadh Massawe alipokuwa akiwaeleza Wabunge wa Jumuiya ya
Afrika Mashariki namna TPA inavyofanya kazi, amesema kuwa kwa mwaka
2013/2014 mizigo inayosafirishwa kutoka bandarini hapo imeongezeka
kutoka tani milioni 4.05 mwaka 2012/13 hadi tani milioni 4.45 mwaka
2013/2014 ambayo ni sawa na asilimia 9.8.
Massawe amesema kuwa mizigo hiyo
ilisafirishwa kutoka bandari ya Dar es salaam kwenda nchi za Zambia,
Jamhuri ya Kidemokrasia Kongo, Burundi, Rwanda, Malawi and Uganda kwa
kutumia mifumo ya barabara na reli.
No comments:
Post a Comment