Pages

KAPIPI TV

Saturday, August 17, 2013

MRABA WA MAGGID:"AZUNGUMZIA TUENDAKO,AMTAJA PIA MAREHEMU MAMA MOSI TAMBWE"


maggid001bc 6b63b
Watanzania hawajachoka kuishi kwa amani, lakini...

KATIKA dunia hii kila jambo hutanguliwa na ishara. Nimepata kuandika, kuwa Afrika mvua hainyeshi ghafla, utaziona ishara za mawingu.

Na nchi nayo ni hivyo hivyo, ishara za nchi inayoelekea kubaya huonekana mapema. Wahenga walituambia, kuwa ukiona zinduna na ambali iko nyuma.

Naingiwa na shaka juu ya kuongezeka kwenye jamii, kwa kauli zenye kuashiria shari zaidi kuliko maridhiano. 

Na wananchi hawako katikati ya hili, bali baadhi ya wanasiasa na wakati mwingine viongozi wa dini.



Ukweli Watanzania walio wengi hawajachoka kuishi kwa amani, bali, kuna baadhi ya wanasiasa na hata viongozi wa dini, kwa kutanguliza maslahi yao, wanahangaika kupandikiza mbegu za chuki miongoni mwa Watanzania. Kwamba Watanzania wabaguane kwa misingi ya udini, siasa na hata ukabila.

Juzi nimeandika makala kuzungumzia hatari ninayoiona katika hili la vyama vya siasa kuanzisha vikosi ama vikundi vya ulinzi. Na ukweli ni kuwa, huko nyuma niliandika juu ya hatari hii katika makala zaidi ya mbili za magazetini, ni kuanzia mwaka 2001 pale CUF na CCM Zanzibar walipokuwa kwenye msuguano mkubwa. Nikaandika tena baada ya Uchaguzi Mdogo wa Arumeru Mashariki pale CCM na CHADEMA walipokwaruzana.

Na hapa nitarejea moja ya mazungumzo muhimu ya kihistoria kupata bahati ya kuyafanya; ilikuwa ni jioni ya Januari 24, 2012 pale nilipokutana na Mama Mosi Tambwe ( sasa marehemu) nyumbani kwake Tabora Mjini.

Mosi Tambwe aliingia TANU akiwa na miaka 18. Ni mmoja wa wanawake mahiri sana kisiasa wa enzi hizo. Mosi Tambwe alinisimulia, kuwa alianzia kwenye TANU Bantu Group, hiki kilikuwa ni kikundi cha vijana ndani ya TANU, ambacho baadaye kikawa TANU Youth League.

Kwa kirefu kabisa Mosi Tambwe aliniambia majukumu yao kama vijana kwa wakati huo. Ni wakati nchi ikiwa chini ya mkoloni. Akanielezea pia majukumu hayo yalivyobadilika baada ya uhuru. Enzi hizo vijana walikuwa wakiandaliwa kupitia TANU Youth League ili waje kuwa makada wa chama, hivyo basi, viongozi wa wananchi walinolewa vema. Walijengewa uwezo wa kujenga hoja.

Ni enzi hizo, baada ya kutoka Chipukizi, hatua iliyofuata ni Tanu Youth League. Wengine wakaenda JKT na hata Jeshini. Azma kubwa ilikuwa kujenga Uzalendo na Umoja wa Kitaifa.

Tumekosea wapi?
Jibu; ni pale, kwa shinikizo la mabadiliko ya dunia , na kwa shingo upande, chama tawala kiliporidhia kurejesha mfumo wa vyama vingi mwaka 1992. CCM ikasahau kuratibu mabadiliko makubwa ya kikatiba ambayo yalipaswa yaendane na mabadiliko hayo ya kimfumo.

Kimsingi, hali tuliyo nayo sasa ya kuchanganyikiwa, hata kwenye hili la vyama kuunda vikosi au la, inatokana na makosa makubwa, kama Taifa, tuliyoyafanya mwaka 1992. Maana, ' Green Guards' katika mfumo wa chama kimoja huenda haikuwa tatizo kubwa.

Nimeandika mara kadhaa, kuwa historia ni mwalimu mzuri, lakini, wakati ni mwalimu mzuri pia. Tujifunze kutokana na mabadiliko ya wakati. Katika wakati tulio nao sasa, vyama vya siasa havipaswi kujiundia vikundi vya ulinzi vyenye kupata hata mafunzo ya kijeshi. Ni ujasiri, kama viongozi wa sasa watazipa mgongo fikra hizi za kizamani na kuendana na mabadiliko ya wakati.

Tufanye nini?
Kama ningeombwa ushauri hii leo, basi, ningevishauri vyama vya siasa, kuwa kwa haraka sana, viachane na harakati za kuunda vikosi au vikundi vya ulinzi. Jukumu hilo liachiwe vyombo vya usalama, hususan Jeshi la Polisi, na hata makampuni ya ulinzi yenye kutambulika kisheria.

Na vile vilivyopo vivunjwe. Maana, vikundi hivi vya ulinzi ambavyo kimsingi ni vikundi vya wanamgambo wa vyama ni maafa tunayoyaandaa wenyewe. Kama hatutanguliza busara na hekima, basi, itakuwa ni suala la wakati tu kabla hatujajikuta kwenye dimbwi la maafa makubwa. 

Tumeshaziona ishara.
Majuzi nilikuwa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam kufuatilia kongamano la Amani ya Nchi yetu kwa miaka 50 ijayo. Kwa masikitiko makubwa, ukumbi ule wa Nkrumah haukujaa vijana.

Kwa vyama vya siasa, badala ya kutumia muda na rasilimali zao kufyeka mapori ya kuwaweka vijana kwenye ' makambi ya ukakamavu', umefika wakati sasa wa kubadilika, kuachana na fikra hizo za kijima zenye kuturudisha nyuma miaka 50.

Huu ni wakati wa kuwajengea vijana wa vyama ' ukakamavu wa akili'. Na mahali kama pale Nkrumah Hall ndipo vijana wa vyama walipaswa wahamasishwe waende wakanoe akili zao. Waende wakajifunze kujenga na kubomoa hoja za wengine kwa nguvu za hoja na si hoja za nguvu.

Zimepita, zama za ' Umkhoto we Sizwe'. Hizi ni zama za ' Umkhoto we Mitwe'- Ni mapambano ya kutumia vichwa kwa maana ya akili.
Naam, ukiona zinduna na ambali iko nyuma.

No comments: