Pages

KAPIPI TV

Friday, January 23, 2015

WANACHAMA WA FIBUCA TAWI LA ATTT WALALAMIKIA VITISHO TOKA KWA MWAJIRI WAO

Mkuu wa wilaya ya Tabora mjini Bw.Suleiman Kumchaya akizungumza  na baadhi ya wanachama FIBUCA tawi la kampuni ya ununuzi wa tumbaku nchini ATTT wakati wa semina fupi ya masuala ya uongozi iliyofanyika Tabora mjini.
Katibu wa FIBUCA mkoa wa Tabora Bw.Ramadhani Wakulichombe akisoma taarifa fupi ya maendeleo ya FIBUCA ambapo alieleza kuwa wanachama wa chama hicho wamekuwa wakikabiliwa na changamoto mbalimbali hususani za kutishwa na viongozi au waajiri katika maeneo yao ya kazi wakati wanapotetea haki za wafanyakazi ambao kimsingi ni wanachama wa FIBUCA.


 Na Juma Kapipi,Tabora.
CHAMA cha wafanyakazi wa asasi za fedha,viwanda,Benki,Uzalishaji wa nishati,Biashara na Kilimo FIBUCA tawi la Tabora kimelalamikia hatua za vitisho wanavyopatiwa wanachama wa chama hicho tawi la kampuni ya tumbaku ya ATTT kutoka kwa mwajiri wao na kusababisha baadhi ya wanachama kutaka kujitoa kwa kuhofia kupoteza ajira zao.

Akisoma taarifa fupi mbele ya kaimu mkuu wa mkoa wa Tabora Suleiman Kumchaya wakati wa semina ya viongozi wa tawi la  chama hicho  katika  kampuni  ya ATTT,Katibu wa FIBUCA mkoani hapa Ramadhani Wakulichombe alisema moja kati ya changamoto  kubwa  inayowakabili ni pamoja  na vitisho dhidi  ya  wanachama na viongozi wa tawi hilo.

Wakulichombe amebainisha  kuwa licha ya FIBUCA kuendelea kujitangaza  sehemu mbalimbali za waajiri na kufanikiwa kuingiza wanachama wengi ikiwemo wafanyakazi wa kampuni ya Association of Tanzania Tobacco Traders ATTT,lakini jambo la kushangaza ni kuona  uongozi wa kampuni ya ATTT ikihoji kwanini wafanyakazi hao wamejiunga na chama hicho jambo ambalo limekuwa likiwatishia na hata kufikia hatua ya kuanza kujitoa wakihofia kupoteza ajira.

Alisema hatua ya kampuni ya uongozi wa kampuni ya ATTT kutishia wanachama ni kinyume na sheria ya ajira na mahusiano kazini sehemu ndogo 'd' inayozungumzia uhuru wa kujumuika(Employees right to freedom of association)kifungu namba tisa(9) kwamba kila mwajiriwa anayo haki na kujiunga na chama cha wafanyakazi anachokiona kinamfaa.

Hata hivyo Katibu huyo wa FIBUCA ameiomba Serikali ya mkoa wa Tabora kuingilia kati na kulifanyia kazi suala hilo ambalo linawafanya wafanyakazi au wanachama wa chama hicho tawi la ATTT kutokuwa na uhuru wa kisheria katika maeneo yao ya kazi.

Akifungua semina hiyo kaimu mkuu wa mkoa wa Tabora Suleiman Kumchaya aliwataka vingozi wa FIBUCA kusimama imara wakati wanapotetea haki za wanachama wao pasipo kuvunja sheria.

Kumchaya alisema vitisho imekuwa ni jambo ambalo linalotumiwa sana na baadhi ya waajiri ikiwa ni moja ya hatua ya kuwanyonya wafanyakazi mahala pa kazi ili wao waweze kunufaika zaidi.

Aidha katika hatua nyingine baadhi ya wafanyakazi wa ATTT ambao hawakutaka kutaja majina yao wameeleza kuwa mwajiri wao amekuwa akilazimisha  wafanyakazi wake wajiunge  na chama cha Wafanyakazi wa Mashambani na Kilimo TPAWU ambacho wamedai kuwa kimekuwa kikilinda zaidi maslahi ya mwajiri kuliko mfanyakazi.

Walisema TPAWU ni chama ambacho kilikuwepo tangu awali kabla ya FIBUCA na hivyo wamedai kuwa kimeshindwa kutetea maslahi ya wafanyakazi ndio maana wakaamua kujiunga na FIBUCA ambacho mwajiri hakubaliani nacho na ndio sababu ya kuwepo kwa vitisho kwakuwa chama hicho kimekuwa kikiweka wazi na kutoa elimu ya haki za wafanyakazi na namna ya kuzidai.

Chama cha wafanyakazi FIBUCA ni chama huru kilichoanzishwa kwa mujibu wa sheria ya ajira na mahusiano kazini namba sita(6)ya mwaka 2004 na kupata usajiri wa kudumu mnamo tarehe 24 Julai 2009 kwa kupewa cheti namba 24 ambapo kilianzishwa na wafanyakazi wapatao 20 kutoka Benki ya NMB,NBC,NSSF na DAWASCO. 
     





No comments: