Pages

KAPIPI TV

Tuesday, October 21, 2014

JK ACHANGIA KITUO CHA VIJANA SIKONGE MIL. 10


Na Mwandishi wetu, Tabora

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr Jakaya Mrisho Kikwete ameahidi kuchangia kiasi cha sh milioni 10 na trekta moja kwa Kituo chaVijana cha Pathfinder Green City kilichoko  wilaya ya Sikonge mkoani Tabora.

Aliitoa ahadi hiyo alipotembelea kituo hicho chenye vijana wapatao 100 ambao wanajifundishwa utaalamu wa aina mbalimbali ikiwemo ufundi, ujenzi, ufyatuaji matofali ya kisasa (aina ya interlock), kilimo, ufugaji nyuki, ufugaji wa kuku na ng’ombe na ujasiriamali.

Rais alionyeshwa dhahiri kufurahishwa na shughuli za uzalishaji mali zinazofanywa na vijana hao sambamba na kujishughulisha na kilimo cha mazao mbalimbali kama vile tumbaku, mahindi, mpunga na mbogamboga ambapo tayari wameshaanza kujipatia kiasi kikubwa cha fedha kutokana na mauzo ya mazao hayo.

‘Kazi niliyokuta kwenye kijiji cha mfano pale Sikonge imenifurahisha sana, wanafanya mambo makubwa, wanalima tumbaku, mahindi, wanafuga nyuki, kuku, ng’ombe, wanashona viatu, nguo, wanafyatua tofali na kujenga nyumba za kisasa wao wenyewe, hawa vijana ni mfano wa kuigwa, wanastahili pongezi’, alisema.

Nimeahidi kuwasaidia shilingi milioni 10 na trekta ili wafanye kilimo kilicho bora zaidi kitakachowafanikisha kiuchumi wao wenyewe, familia zao, jamii inayowazunguka, wananchi wa wilaya ya Sikonge, mkoa mzima wa Tabora na taifa kwa ujumla, aliongeza.

JK alibainisha kuwa vijana walioko katika kituo hicho kilichoko katikati ya vijiji vya Lufwisi na Tumbili wilayani humo watakuwa mfano wa kuigwa na waalimu wazuri kwa wenzao na jamii nzima kwani mafunzo wanayopata yanawapa ujuzi mkubwa sana katika kilimo na fani nyinginezo.

Aidha JK alipongeza uongozi wa halmashauri ya wilaya hiyo chini ya Mkuu wa wilaya Hanifa Selengu na Mkurugenzi Mtendaji Shadrack Mhagama na serikali ya mkoa huo kwa kufanikisha uanzishwaji kituo hicho cha mfano katika mkoa huo huku akiwataka waendelee kukisimamia vizuri zaidi.

Aidha akiwa katika ziara hiyo aliziagiza halmashauri zote hapa nchini kujiwekea utaratibu wa kutoa taarifa za maendeleo mara kwa mara angalau kila baada ya miezi nne ili kubaini mafanikio yako wapi na changamoto ni zipi ili waweze kuweka utaratibu wa namna ya kukabiliana nazo, kwa kuanzia aliwataka kutoa taarifa za maendeleo mwezi desemba na nyingine baada ya miezi 4.

No comments: