Mwenyekiti wa Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, ameonya kuwa iwapo
kiongozi yeyote wa chama hicho ataruhusu mgombea wa Chama Cha Mapinduzi
(CCM) wa ngazi yoyote ya uongozi katika uchaguzi, kupita bila kupingwa
katika eneo lake, atawajibika.
Alitoa onyo hilo alipokuwa akifungua Mkutano Mkuu wa Bavicha, jijini Dar es Salaam jana.
“Misiruhusu uongozi, kuanzia
serikali ya mtaa kupita bila kupingwa. Ikitokea hivyo, na wewe kiongozi
(wa Chadema) jiandae kuwajibika,” alisema Mbowe.
Aliutaka uongozi mpya wa Bavicha utakaochaguliwa kuendeleza kazi nzuri iliyoachwa na uongozi wa baraza hilo uliopita.
Kazi hizo ni pamoja na namna ya
kuwaandaa vijana, wazee na wanawake, kujiandikisha kwenye daftari la
kudumu la wapigakura na kushiriki chaguzi zote, kuanzia ule wa serikali
za mitaa, vijiji na vitongoji, udiwani, ubunge na urais mwakani.
Mbowe, ambaye pia ni Mwenyekiti wa
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) alisema muda mwafaka ukifika,
watakutana na viongozi wenzake wa vyama vinavyounda umoja huo vya CUF na
NCCR-Mageuzi kuangalia namna watakavyofanya kazi pamoja katika chaguzi
zijazo.
Alisema kifungu cha 6 (3) na (4)
cha katiba ya Chadema kinaelezea ukomo wa uongozi, hivyo akasema wana
kazi kubwa ya kupanua wigo wa chama.
Kwa kuzingatia hilo, alisema watakuwa na kazi ya kutathmini
utendaji wa kila kiongozi katika chama kila baada ya miezi sita kuona
namna alivyochangia kukuza na kukiimarisha chama.
“Kiongozi atakayeruhusu katika eneo lake chama kisikue, atawajibika kabla ya miaka mitano,” alisema Mbowe.
Alisema Chadema siyo ya fujo, bali
ni chama chenye dhamira ya kweli, hivyo akaonya kuwa iwapo mwanachama
wake yeyote anayegombea uongozi kwa kutumia mbinu chafu, ikiwamo rushwa,
atang’olewa hata kama atakuwa amekwishakupitishwa katika uchaguzi.
Awali, akimkaribisha Mbowe
kufungua mkutano huo, Mwenyekiti wa Bavicha anayemaliza muda wake, John
Heche, alisema Chadema imekua na kwamba, kigezo cha hilo ni namna
ilivyofanikiwa kufanya kwa mara ya kwanza uchaguzi, kuanzia ngazi za
msingi.
Aliushukuru uongozi wa Chadema kwa
kuwashughulikia wasaliti ndani ya chama na kusema kamwe vijana
hawatavumilia kuona mtu yeyote anakivuruga chama hicho.
Mapema, Katibu Mkuu wa Bavicha
anayemaliza muda wake, Deogratius Munishi, alisema wajumbe waliotakiwa
kuhudhuria ni 336 na kwamba, hadi kufikia saa 5.40 asubuhi,
waliosajiliwa walikuwa 301 sawa na asilimia 89 ya akidi ya wajumbe wote
wa mkutano huo.
No comments:
Post a Comment