Pages

KAPIPI TV

Sunday, August 31, 2014

CHUO CHA MAFUNZO YA NYUKI TABORA KUPANDISHWA HADHI

Waziri wa maliasili na Utalii Lazaro Nyalandu katika picha ya pamoja na Wahitimu wa mahafali ya tatu Chuo cha Nyuki Tabora

Na Allan Ntana, Tabora

SERIKALI imeahidi kupandisha hadhi ya Chuo cha Mafunzo ya Nyuki kilichoko mkoani Tabora ili kuwavutia wanafunzi wengi zaidi kutoka ndani na nje ya nchi kujiunga na chuo hicho.

Hayo yalibainishwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Razaro Nyarandu aliyekuwa mgeni rasmi katika mahafali ya 3 ya Chuo hicho yaliyofanyika juzi chuoni hapo.

Alisema kutokana na umuhimu wa Chuo hicho atahakikisha kinaboreshwa zaidi ili kiwe kitovu cha ubora katika taaluma ya sayansi ya misitu na nyuki na hifadhi zake na kwa kuanzia ameahidi kuwasiliana na wataalamu wa wizara hiyo ili wahuishe mitaala yake ili kukiongezea hadhi.

‘Tunataka chuo hiki kiwe kimbilio la wanafunzi kutoka sehemu mbalimbali hapa nchini na hata nje ya nchi, tutakiboresha zaidi ili kiwe kitovu cha ubora katika sayansi ya misitu na nyuki’, alisema Waziri Nyarandu.

Aliongeza kuwa Wizara yake itajitahidi kuzishughulikia changamoto zote zinazokikabili ikiwemo suala la upungufu wa watumishi ili kuhakikisha chuo hicho na sekta zingine zilizoko ndani ya Wizara hiyo zinakuwa na watumishi wa kutosha sambamba na kutoa fursa za ajira kwa askari wa wanyama pori na wataalamu wengineo.

Lengo ni kuhakikisha ulinzi wa kutosha unakuwepo katika maeneo yote ya hifadhi za misitu sambamba na kuwezesha shughuli zingine zote ziendelee vizuri katika maeneo hayo ikiwemo ufugaji nyuki.

Awali akisoma risala ya Chuo mbele ya Waziri, Mkuu wa Chuo hicho Semu L. Daud alisema tangu Mafunzo ya Chuo hicho yarudishwe rasmi mkoani Tabora chuo hicho kimeanza kupata mafanikio makubwa ikiwemo kuongeza udahili wa wanafunzi  kutoka 34 kwa mwaka 2010/2011 hadi 115 kwa mwaka 2014/15, huku akibainisha kuwa wanafunzi 58 wa kike na kiume kwa mwaka 2013/14 wamehitimu mafunzo hayo katika ngazi ya Astashahada na Stashahada ya Ufugaji Nyuki .

Alitaja mafanikio mengine kuwa ni pamoja na Chuo kupata utambulisho maalumu toka Baraza la Elimu ya Ufundi (NACTE) wa Ithibati ya muda (Partial Accreditation), ili kuthibitisha umuhimu wa taaluma inayofundishwa na Chuo hicho wamepewa fursa ya kushiriki katika Maonyesho ya Biashara na Kilimo (Sabasaba na NaneNane) kuanzia mwaka 2009 mpaka sasa ili kuelimisha wananchi.

Aidha Mkuu wa Chuo alitaja changamoto mbalimbali zinazokikabili chuo hicho kuwa  pamoja na upungufu wa watumishi wasio wakufunzi hususani Afisa Utumishi, Wakutubi, Wapishi, Madereva, Afisa Ugavi, walinzi na mwangalizi wa masijala.

Changamoto nyingine ni tatizo la uhaba wa vifaa vya kisasa vya kufundishia ikiwemo vitabu na chombo cha usafiri hasa kwa shughuli za utawala na shughuli za mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi.

Aidha alibainisha kuwa hadhi ya Chuo hicho itaongezeka pale tu mikakati yote ya kukipanua na kukiboresha itakapotekelezwa ipasavyo hivyo akaiomba serikali kupitia Waziri mwenye dhamana kuangalia uwezekano wa kuongeza fungu la bajeti ya Chuo hicho ili jitihada za kuboresha miundombinu hiyo zianze mra moja.


No comments: