Baadhi ya
wananchi wa Manispaa ya Iringa leo wameamka asubuhi na mapema kwenda
maeneo mbali mbali ambayo usiku wa kuamkia jana senene wengi zaidi
walianguka.Licha ya wananchi hao kuchukua jitihada kadhaa za kusaka kitoweo hicho kinachopatikana mara moja kwa mwaka, leo hii wamejikuta wakiambulia patupu kufuatia kukosekana kwa wingi kwa wadudu hao hali iliyosababishwa na ukosefu wa miundo mbinu ya taa ambayo ni kivutio kikubwa cha wadudu hao.
Imeelezwa kuwa baadhi ya wamiliki wa nyumba zinazowasha taa usiku kwa ajili ya ulinzi binafsi wa nyumba hizo katika manispaa ya Iringa hawakuwa wamewasha taa na hivyo kusababisha wadudu hao kushindwa kufika na kutokuwa rahisi kwa wananchi kuwapata.
Uchunguzi wa mtandao huu umebaini hali hiyo baada ya kuzunguukia maeneo mbali mbali maarufu ambayo jana Senene walianguka na kusababisha kuwepo kwa msongamano mkubwa wa wananchi ambao walifika kukusanya senene hao.
Baadhi ya watu waliokutwa katika jengo la Asas eneo la Ngangilonga kwenye barabara kuu ya Iringa - Dodoma walisema kuwa walilazimika kufika mapema eneo hilo ili kuokota senene ila cha kushangaza baada ya kufika hao walishuhudia giza nene na hakuna senene wanaoanguka hapo hali iliyowakosesha kitoweo hicho.
Zaidi ya watu 20 waliokutwa hapo asubuhi majira ya saa 11;30 asubuhi ya leo walikuwa na mifuko mikubwa ya naironi kwa ajili ya kukusanya senene na kwenda kuwauza na baadhi yao kusaka kitoweo hicho.
Pamoja na jengo hilo la Asas kukosa mwanga na kuwa giza kiasi cha senene kushindwa kuanguka bado maeneo mbali mbali ya uhindini ambayo jana senene wengi zaidi walianguka leo hali imekuwa tofauti zaidi baada ya senene kutoanguka kwa wingi.
Hata hivyo baadhi ya walinzi wanaolinda katika eneo hilo la Asas na maeneo mengine ambayo jana yaliongoza kwa kuanguka senene wengi zaidi wamedai kuwa wenye nyumba hizo waliamua kuzima taa ili kuepusha uchafu wa kuta zao na maeneo yao kama ilivyojitokeza jana .


No comments:
Post a Comment