Pages

KAPIPI TV

Wednesday, September 19, 2012

SERIKALI YATAKIWA KUUNGA MKONO JITIHADA ZA WADAU KUTOKOMEZA AJIRA MBAYA KWA WATOTO

Na Allan Ntana, DSM
 

Serikali imetakiwa kuunga mkono jitihada zinazofanywa na wadau mbalimbali kwa kushirikiana na taasisi za hapa nchini katika kupiga vita utumikishwaji wa watoto katika shughuli mbalimbali za kiuchumi kwani hali hii inawakandamiza watoto ikiwa ni pamoja na kuwanyima haki zao za msingi za kielimu.
 
Hayo yalibainishwa na wadau mbalimbali waliohudhuria katika mkutano wa siku moja uliofanyika juzi katika ukumbi wa White Sands Hotel ulioko Kunduchi jijini Dar es salaam, ambapo wadau hao kwa kauli moja waliitaka serikali kuunga mkono juhudi zote zinazofanywa na wadau hao ili kuhakikisha suala zima la utumikishwaji wa watoto katika ajira mbaya linatokomezwa.
 
Mkutano huo wa pili wa kitaifa ulioandaliwa na  taasisi ya PROSPER ulilenga kuwakutanisha  wajumbe wote wa kamati ya ushauri ya taasisi hiyo (Prosper National Advisory Committee) na wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na watendaji kutoka serikalini ili kuzungumzia mikakati ya namna ya kupambana na kuzuia utumikishwaji wa watoto katika ajira mbaya hasa kwa wakulima wa zao la tumbaku.
 
Akitoa taarifa  katika mkutano huo, Mkurugenzi Mtendaji wa mradi wa PROSPER Bw. Bahati Nzunda alisema kuwa mkutano huu ni mahsusi kwa ajili ya kuzungumzia mapana ya tatizo hili la ajira mbaya kwa watoto ili kurahisisha harakati zake, kwani viongozi walio wengi bado hawajawa na ufahamu wa kutosha wa kuweza kutofautisha juu ya kazi anazopaswa kushirikishwa mtoto na zile ambazo hapaswi kushirikishwa ili kutoathiri haki zake za msingi.
 
Aidha Bw. Nzunda aliongeza kuwa mradi wa PROSPER tayari umeshachukua hatua kwa kuanzisha miradi kadha wa kadha  ili kuwakomboa watoto wanaotumikishwa katika mashamba ya tumbaku katika wilaya za Urambo na Sikonge mkoani Tabora.
 
Aidha Bw. Nzunda alisema kwamba zoezi hili limeonyesha mafanikio makubwa sana kwani watoto wengi waliokuwa wamenyimwa haki ya kusoma shule tayari wamepelekwa shule kwa ufadhiri wa mradi huu, na wale waliomaliza darasa la saba  na kushindwa kuendelea wameanzishiwa miradi ya kilimo na ujasiriamali kwa vikundi mbalimbali vya akina mama.
 
 ‘‘……tunaomba serikali ituunge mkono katika hili ili kurahisisha jitihada zetu, naamini  wizara zikishirikiana na sisi kwa moyo wa dhati, tutafanikiwa kutokomeza utumikishwaji huu na kutokomeza umaskini kwa wazazi wa watoto hawa,’’ aliasa Bw. Nzunda.
 
Akichangia mada katika mkutano huo, Mkurugenzi wa sera wa mradi wa PROSPER, Bi. Mary Kibogoya, alisema kuwa tatizo la ajira kwa watoto linazidi kuwa kubwa na linasababishwa na umaskini wa familia zilizo nyingi hapa nchini, jambo ambalo limewafanya watoto wengi kuendelea kukimbilia katika ajira hizi za mashamba ya tumbaku hasa kutoka mikoa ya Kigoma, Tabora, Singida, Katavi, na Rukwa.
 
Bi. Kibogoya aliongeza kuwa mkutano huu utaleta mwamko mpya kwa kila mmoja wetu juu ya nini kifanyike na hatimaye kuunganisha nguvu ya pamoja ili kutokomeza utumikishwaji huu wa watoto, na akatoa wito kwa serikali na wadau mbalimbali  kuunga mkono jitihada zinazofanywa na mradi wa PROSPER ili kutokomeza ajira hizi mbaya kwa watoto.
 
Naye Bi. Cindy Serre ambaye ni Meneja miradi wa taasisi ya ECLT toka Geveva, nchini Uswisi, ambao ni wafadhiri wa mradi wa PROSPER hapa nchini, alisema kuwa lengo la mkutano huu ni kuifanya serikali na wadau wengine wajue ukubwa wa tatizo hili la utumikishwaji wa watoto na  kuweka mikakati ya nini kifanyike  ili kutokomeza hizi ajira mbaya na kuboresha maisha ya watoto hawa, lakini hili haliwezi kufanikiwa pasipo serikali kuunga mkono jitihada hizi.
 
Mkutano huo ulihudhuriwa na Mkurugenzi Mtendaji wa mradi wa PROSPER Bw. Bahati Nzunda, Meneja wa Sera Bi. Mary Kibogoya na maofisa waandamizi wa mradi huo kutoka mkoani Tabora, wengine ni   Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya Urambo Bw. Adam Malunkwi na Mwakilishi wa Shirika la kazi duniani  (I.L.O) Bi. Noreen Toroka.
 
Wengine ni Mkurugenzi mkuu wa taasisi ya ECLT toka Geneva , Uswisi, Bi. Sonia Velazquez, Ofisa Mkuu–Mipango wa taasisi ya Winrock International toka Marekani, Bi. Vick Walker, Meneja miradi wa ECLT toka Geneva , Uswisi, Bi. Cindy Serre, wawakilishi wa taasisi na makampuni ya tumbaku hapa nchini na maofisa toka serikalini waliowakilisha wizara mbalimbali. 
 

No comments: