Pages

KAPIPI TV

Monday, March 23, 2015

23 UYUI WAHITIMU MAFUNZO YA WASAIDIZI WA KISHERIA VIJIJINI

    
Katibu Msaidizi wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Magharibi Bw.Salvatory Kilasara akitoa maada ya maadili ya viongozi wa Umma wakati wa kuhitimisha  mafunzo ya Wasaidizi wa kisheria wilaya ya Uyui yaliyofanyika kwa muda wa siku 25.
Baadhi ya Wasaidizi wa kisheria wakipokea vyeti vya kuhitimu Mafunzo ya Sheria mbalimbali za nchi.




Tabora

JUMLA ya vijana 23 wakiwemo wanawake 9 na wanaume 14 wamehitimu mafunzo maalumu ya ‘Wasaidizi wa Kisheria’ vijijini yaliyoendeshwa katika wilaya ya Uyui mkoani Tabora na taasisi ya Jamii Salama Development Volunteers (JSDV) yenye makao yake makuu mjini Tabora.

 Mafunzo hayo yaliyofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Denmark (DANIDA) kupitia Mfuko wa Huduma za Kisheria (Legal Services Facility-LSF) yaliendeshwa kwa muda wa siku ishirini na tano (25) chini ya usimamizi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (Tanganyika Law Society).

Akizungumza katika hafla ya kufunga mafunzo hayo jana, Katibu Msaidizi wa Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda ya Magharibi Bw.Salvatory Kilasara alisema mafunzo waliyopata vijana hao ni msaada mkubwa kwa jamii hasa kule vijijini ambako wananchi walio wengi hawana mtu wa kuwapa mwongozo au msaada wa kisheria utakaowawezesha kupata haki zao kama inavyostahili.

Ili wafanikiwe katika kazi hiyo ya utoaji msaada wa kisheria kwa wananchi ikiwemo kusuluhisha migogoro ya wananchi hususani kule vijijini, Kilasara aliwataka wahitimu hao kuwa waadilifu, kufanya kazi kwa weledi, kuweka mbele maslahi ya jamii na kuendelea kujifunza zaidi kwa wanasheria wengine.

Aliwataka kuongeza mshikamano zaidi na taasisi ya JSDV, halmashauri ya wilaya Uyui na jamii kwa ujumla, aidha aliasa vijana hao kusaidia kuelimisha jamii juu ya utokomezaji vitendo vyote vya ukatili na unyanyasaji kijinsia ikiwemo vitendo vya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi.

Mwakilishi wa Tanganyika Law Society (TLS) Seleman Pingoni alipongeza jitihada na utayari wa vijana hao kuitetea jamii inayowazunguka, hivyo akawataka wasiwe watendaji wa ofisini tu bali wawatembelee wananchi mbalimbali kule vijijini na kutoa mwongozo wa elimu ya sheria katika jamii na sio kuwa mahakimu.

Naye Mkurugenzi Mkazi wa JSDV Pascal Kilagula alisema vijana hao sasa wameiva na wako tayari kuitumikia jamii na kama taasisi wana matarajio makubwa juu yao, hivyo akawataka kuonyesha ufanisi wa hali ya juu.

Aidha Kilagula alibainisha kuwa mkakati wa kuanzisha kituo cha sheria katika kijiji cha Isikizya wilayani Uyui kwa ajili ya kuwasaidia wananchi uko mbioni kuanza na kituo hicho kitaendeshwa na vijana hao waliohitimu mafunzo ya msaada wa kisheria chini ya usimamizi wa TLS.

Awali akisoma risala kwa niaba ya wahitimu wenzake Bi.Theresia Kyejo alieleza kuwa wamepata elimu na uelewa wa kutosha utakaowasaidia kutoa msaada wa kisheria kwa jamii na sasa wana ujasiri na ari kubwa ya kuwatumikia wananchi hasa baada ya kufanikiwa kutatua na kusuluhisha jumla ya migogoro 340 katika kata mbalimbali wilayani humo katika kipindi cha mafunzo hayo.

No comments: