Pages

KAPIPI TV

Tuesday, April 29, 2014

ASKARI WANNE NA RAIA 14 WAPOTEZA MAISHA KATIIKA AJALI YA GARI SINGIDA


Untitled
Baadhi ya miili ya wakazi wa kijiji cha Utaho wilaya ya Ikungi, waliogongwa na basi la Summry ikiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali ya mkoa wa Singida mjini humo.
DSC08054
Baadhi ya ndugu na jamaa wakiwa wanatafakari juu ya ndugu zao kugongwa na basi la summry la kufariki dunia usiku wa kuamkia leo katika kijiji cha Utaho wilaya ya Ikungi.
DSC08077
Baadhi ya ndugu wakiwa nje ya chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali ya mkoa mjini Singida,wakisubiri kuchukua miili ya ndugu zao waliogongwa na basi la Summry.(Picha na Nathaniel Limu).

Na Nathaniel Limu wa MOblog, Singida
ASKARI Polisi wanne wa kituo cha Polisi Singida mjini na wakazi 14 wa kijiji cha Utaho tarafa ya Ihanja wilaya ya Ikungi mkoani Singida,wamefariki dunia baada ya kugongwa na basi la kampuni ya summry T.799 BET aina ya nissan.

Tukio hilo limetokea Aprili 28 mwaka huu saa 2.45 usiku katika barabara kuu Singida-Dodoma eneo la kijiji cha Utaho wilaya ya Ikungi.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoa wa Singida,SACP.Geofrey Kamwela askari hao ni F.849 D/CPL Boniface Magubika,F.6837 Pc Jumanne Mwakihamba,G.7993 Pc Novatus Tarimo na G.8948 Pc Michael Mwakihaba.

Alitaja wengine waliofariki kuwa ni pamoja na Ramadhani Mjengi afisa mtendaji wa kijiji cha Utaho,Paul Hamisi mwenyekiti wa kijiji cha Utaho,Ernest Salanga,mwenyekiti wa kitongoji cha Utaho,Saidi Rajabu,Usirika Itambu,Chima Mughenyi,Slim Juma,Abeid 
 Ramadhani,Mwinyi Hamisi na Issa Husein wote wakazi wa kijiji cha Utaho.

Aidha.Kamwela amesema kuwa miili ya watu wengine bado haijatambuliwa na imehifadhiwa kwenye chumba cha maiti cha hospitali ya mkoa mjini Singida.

Akizungumuzia juu ya ajali hiyo,kamanda huyo amesema kuwa awali kijana Gerard Zephania (24) akiwa ametoka kusaga nafaka aligongwa na gari la mizigo ambalo bado halijafahamika na kufariki papo hapo.

“Askari wa polisi wakitumia gari PT 1424,walifika eneo la tukio kwa ajili ya kuubeba mwili wa Gerard kuuleta katika hospitali ya mkoa kwa uchunguzi,kundi la wananchi wa kijiji cha Utaho nao walifika eneo la tukio”,amesema na kuongeza;

“Wakati askari polisi wakiwa kwenye harakati ya kuupakia mwili huo ghafla basi la summry liliacha njia na kuingia kushoto mwa barabara kwa nia ya kulikwepa gari la polisi na ndipo lilipovamia na kugonga kundi la watu hao wakiwemo askari polisi.Watu 15 walifariki papo hapo”,amesema Kamwela.

Kamanda Kamwela amesema kuwa dereva wa basi hilo Paulo Njilo mkazi wa Dar-es-salaam hakuweza kusimamisha basi hilo nadi kilomota 25 alipolisimamisha na yeye kutorokea kusikojulikana.

Aidha,amesema ajali hiyo imesababisha majeruhi nane ambapo wawili kati yao wamelazwa katika hospitali ya mkoa na hali zao zinaendelea vizuri.Majeruhi wengine sita wamelazwa katika hospitali ya misioni ya Puma na hali zao sio nzuri.

“Uchunguzi zaidi juu ya ajali hiyo unaendelea ili kujua chanzo halisi cha tukio pamoja na kumtafuta dereva wa basi ili aweze kuhojiwa na kisha hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi yake”,amesema Kamanda Kamwela.

No comments: