Pichani  ni Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa Tanzania Dkt. Alberic Kacou akiongoza wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa kwa kujitolea damu ikiwa ni wiki ya Kampeni ya Kitaifa ya kujitolea damu. Kulia ni Afisa Mtaalam wa damu kutoka Mpango wa Taifa wa Damu Salama Bw. Deochris Kaimukilwa.


Dkt. Alberic Kacou akizungumza na waandsihi wa habari baada ya kumaliza zoezi la kujitolea damu ambapo amezungumzia changamoto Umoja wa Mataifa unazokabiliana nazo katika kufanikisha zoezi la kuhamasisha watu kujitolea damu ambapo ametaja moja wapo kuwa ni ugumu uliopo katika kuwashawishi watu kujitolea kutokana na fikra watu walizonazo kuhusiana na kujitolea damu.

Afisa Mawasiliano wa Umoja wa Mataifa Tanzania Hoyce Temu akifanyiwa vipimo vya awali kabla ya kuchangia damu. Kulia Mtaalamu kutoka mpango wa Taifa wa Damu Salama Bi. Edith Senga.

Hoyce Temu akiandika taarifa muhimu zinazohitajika kabla ya kuchangia damu. Kulia ni Data Clerk kutoka mpango wa Damu Salama Janeth Laswai.

Edith Senga akitoa tathmini kwa waandishi wa habari kuhusiana na zoezi zima la utoaji damu linavyoendelea nchini.
Kauli mbiu ya kuchangia Damu katika kampeni ya kuchangia damu nchini
Taarifa hii kwa hisani ya MO BLOG.
Umoja wa Mataifa umetoa wito kwa watanzania wote kwa ujumla kujitokeza kwa wingi kujitolea damu ili kufanikisha azma ya serikali ya kuwa na damu ya kutosha katika benki ya akiba ya damu.
Akizungumza leo jijini Dar es Salaam katika kituo cha kijitolea damu kilichopo katika zahanati ya UN iliyopo Kinondoni, Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa Dkt. Alberic Kacou amesema Umoja huo unashirikiana bega kwa bega na serikali katika kuhamasisha kampeni ya Mpango wa Taifa wa Damu Salama.

Katika kufanikisha kampeni ya kitaifa ya Kujitolea Damu, Umoja wa Mataifa umeweka utaratibu wa kuwa na vituo katika sehemu mbali mbali ambapo wananchi watakuwa wakijitolea damu, ambapo kwa kuanzia leo kituo kipo katika klinik ya UN ambako kwa kuonyesha mfano Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa Dkt. Alberic Kacou amejitolea damu.
Afisa Mawasiliano wa Umoja wa Mataifa Tanzania Bi. Hoyce Temu akizungumza na MoBlog, amesema kesho tarehe 14 June 2012 ambayo ndio kilele cha Siku ya Kujitolea Damu Duniani, shughuli hiyo itafanyika katika Ofisi za Shirika la Afya Duniani – WHO zilizopo mkabala na Hospitali ya Saratani  ya Ocean Road.

Aidha amewataka wananchi jijini Dar es Salaam kujitokeza kwa wingi ili kufanikisha lengo la Siku ya Kujitolea Damu Duniani, na kuwatoa hofu kuwa sio kweli kwamba ukijitolea damu unapimwa virusi vya ukimwi au damu yako itapungua.

Viongozi katika ngazi mbalimbali na watu wote mashuhuri wanatakiwa kutumia nafasi walizonazo kuhamasisha watu kuchangia damu.