Na Juma Mohammed,MAELEZO
Chama cha Wananchi(CUF) kimewataka wananchi kutulia na Serikali kufanya
uchunguzi wa kina kubaini chanzo cha vurugu zilizotokea mwishoni mwa
wiki Mjini Zanzibar.
Taarifa ya Chama hicho kwa vyombo vya habari iliyotiwa saini na
Mkurugenzi wa Uenezi na Mahusiano na Umma,Salim Bimani ilisema “Chama
cha CUF kinatoa wito kwa wananchi wote kuwa watulivu, wavumilivu na
kuitumia fursa ya kutoa mawazo yao bila jazba na kutowanyima wengine
nafasi ya kuwasilisha mawazo yao”
Taarifa hiyo ilisema kwamba vitendo vya watu wachache kuchoma makanisa
moto na kuharibu mali za watu ni bvya uvunjifu wa sheria na kinyume na
utamaduni wa Kizanzibari.
“Uchunguzi wa kina ufanyike na waliohusika wachukuliwe hatua za
kisheria bila uonevu wala upendeleo” Alisema Bimani katika taarifa yake
hiyo ambayo pia alisema kwamba ni lazima kwa wakati huu na kwa haraka
iwezekanavyo, Serikali izungumze na Mashekhe bila ya kuona muhali na
kwa uwazi kabisa ili kutafuta suluhu ya kudumu kwa faida ya nchi.
Chama hicho kimesema kwamba pamoja na sababu au visingizio mbalimbali
vilivyotajwa kuwa chanzo cha hali hiyo, zikiwemo za hamasa za wananchi,
chuki binafsi, ukosefu wa hekima,matumizi ya nguvu za dola na hata
uchochezi wa makusudi wa wale wanaoonekana kutokupendelea maridhiano ya
kisiasa Zanzibar.
“Chama cha Wananchi,CUF, kama sehemu muhimu ya Umma wa
Watanzania,hakiwezi kukaa kimya kutokana na mwelekeo mzima wa hali tete
ya amani katika nchi, ingawa ni dhahiri wapo baadhi ya watu wasioitakia
mema Zanzibar wakibainika kufurahia mazingira hayo,kwa maslahi binafsi
na pia kutoa kauli za kutatanisha za kisiasa” Alisema Bimani katika
taarifa yake.
No comments:
Post a Comment