Pages

KAPIPI TV

Monday, August 25, 2014

FPCT WAKEMEA VITENDO VYA UKATILI NA MAUAJI YA ALBINO

Na Allan Ntana, Tabora

KANISA la Free Pentecost Church of Tanzania (FPCT) limekemea vikali watu wote wanaojihusisha na vitendo vya ukatili na mauaji dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino) ambavyo vinazidi kushamiri hapa nchini.

Hayo yalijiri jana katika ibada maalumu ya uzinduzi wa kanisa hilo lililopo katika mtaa wa Kilolelini katika Manispaa ya Tabora iliyoongozwa na Askofu Wilson Lazaro ambaye ni Makamu Askofu Mkuu wa FPCT hapa nchini, ibada hiyo iliambatana na tukio la kusimikwa Mchungaji Kiongozi wa kanisa hilo Peter Shani na timu ya watendaji wa kanisa.

Akihubiri katika ibada hiyo Askofu Lazaro alisema vitendo vya ukatili wanavyofanyiwa wanadamu wenye ulemavu wa ngozi havipaswi kufumbiwa macho kwani vinafanywa na watu wasiotaka kutembea na Mungu katika maisha yao hivyo ni lazima tuvikatae na tuvikemee vikali makanisani na nje ya kanisa.

‘Tunakataa vitendo vyote vya ukatili na mauaji dhidi ya albino, katika jina la YESU kristo, watu wote wanaojihusisha na vitendo hivyo popote walipo washindwe…. tunawakemea kwa mamlaka ya jina la YESU kristo’,  haya ni maneno yaliyojiri katika maombi yaliyoongozwa na Askofu Lazaro.

Alisema katika kizazi hiki wanadamu wengi wanampenda sana Mungu lakini tatizo lililopo hawataki kutembea naye katika maisha yao yote na katika shughuli zao za kila siku jambo ambalo linaongeza uadui, chuki na uharibifu mkubwa.

Aidha alifafanua kuwa thawabu, hekima na utajiri vinatoka kwa Mungu na sio kwa wanadamu, japokuwa wanadamu wengine leo hii wanahangaika kutafuta utajiri usiku na mchana kwa waganga wa kienyeji ambao huwaelekeza kwenda kuleta viungo vya albino ili wapate utajiri, hii sio sawa.

‘Tukitaka kufanikiwa ni lazima tutembee na Mungu katika maisha yetu, hata hili kanisa lenu mkitaka baraka zimiminike na mzidi kufanikiwa zaidi ni lazima mtembee na Mungu, kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Waebrania 11:5-6’, alisema.

Akizungumzia mchakato wa kupata katiba mpya unaoendelea hivi sasa hapa nchini Askofu alitoa wito kwa kila Mkristo kumwomba Mungu ili atuwezeshe kupata katiba bora itakayokidhi matakwa ya kila Mtanzania katika nyanja mbalimbali za kiuchumi, kielimu, kisiasa na kijamii.

Awali akisoma risala ya kanisa kwa mgeni rasmi (Askofu Lazaro), Mchungaji Kiongozi wa kanisa la FPCT Parishi ya Tabora Mch.Elias Shijja alisema kanisa la Kiloleni lenye waumini 494 sasa tangu lianzishwe mwaka 1983 limekuwa na mafanikio mbalimbali ikiwemo kuongezeka kwa mapato ya kanisa ambapo yalifikia kiasi cha sh 23,867,600 kwa mwaka.

Alitaja mafanikio mengine kuwa ni pamoja na kupata jengo la kuabudia ambalo sasa liko mbioni kupanuliwa zaidi, kupata waalimu 26 wa shule ya jumapili, wainjilisti 9, mashemasi 16, wazee wa kanisa 4  na kuongezeka watoto wa shule ya jumapili hadi 138 sasa.

Naye Askofu wa kanisa hilo jimbo la Tabora Jeremiah Mnangala alibainisha kuwa kasi ya kukua kwa kanisa hilo katika mkoa huo inaridhisha sana kwani awali walikuwa na parishi mbili tu za Yerusalemu na Ng'ambo na jumla ya makanisa 11 lakini sasa wamepata parishi ya tatu ya Kilolelini na idadi ya makanisa yao sasa imefikia 18.

No comments: