Pages

KAPIPI TV

Sunday, May 27, 2018

UIMARISHAJI MPAKA ARUSHA

01
Bw. Nairoti Kenanda kutoka kijiji cha Njoroi katika tarafa ya Loliondo wilayani Ngorongoro mkoani Arusha akishiriki kuchimba shimo lenye urefu wa mita moja kwa ajili ya kuwekwa alama ndogo ya mpaka wa kimataifa kati ya Tanzania na Kenya unaopita katika kijiji hiko.
02
Wanakijiji wa Kijiji cha Sukenya katika kata ya Soitsambu wilayani Ngorongoro mkoani Arusha wakisoma vipeperushi walivyopewa wakati wa utoaji elimu na uhamasishaji kuhusu uimarishaji wa mpaka wa Kimataifa kati ya Tanzania na Kenya ulioanza mkoani Arusha.
……………..
Na Rehema Isango, Arusha
Jumla ya kilomita 91 za mpaka wa Kimataifa kati ya Tanzania na Kenya mkoani Mara zimeimarishwa na sasa timu za wataalam wa upimaji ardhi na ramani zimeanza kazi hiyo wilayani Ngorongoro katika mkoa wa Arusha.
Kiongozi wa timu ya wataalam kutoka Tanzania Bw. Isaack Marwa amefafanua kuwa jumla ya alama kuu 66 zenye umbile la pembetatu zimeimarishwa ambapo kati ya hizo, 47 zimejengwa upya baada ya kung’olewa na 19 zimekarabatiwa baada ya kuchakaa katika maeneo ya mbalimbali ya wilaya za Rorya na Tarime mkoani Mara.
Amesema kuwa wamefanikiwa kuweka alama mpya ndogo  takriban 900 zenye umbile la pembe nne ambazo zinaonana na kwamba sasa zinawezesha eneo la lote la mpaka wa kimataifa mkoani Mara kuonekana kwa urahisi ambapo kazi hiyo imetumia muda wa mwezi moja na majuma mawili.
Pamoja na kazi ya uwekaji wa alama, pia kazi ya usafishaji wa eneo la mpaka kwa urefu wa mita tano kwa kila upande wa nchi imefanyika  kwa kufyeka miti na kuwezesha alama hizo kuonekana kwa urahisi zaidi.
Bw. Marwa amesema kuwa hivi sasa wameanza kazi mkoani Arusha baada ya kuruka kwa muda eneo la Hifadhi ya Taifa ya Serengeti mkoani Mara lenye urefu wa kilomita 51 kutokana na mvua kuharibu barabara zinazotakiwa kufikisha vifaa vya ujenzi wa alama pamoja na wataalam.   
“Tumelazimika kuendelea na kazi hii katika kijiji cha Ololosokwan kilichopo katika wilaya ya Ngorongoro mkoani Arusha ambacho kimepakana na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti kisha  tutarejea nyuma kumalizia kipande tulichokiruka baada ya njia zinazotusaidia kufikisha vifaa na wataalam hifadhini kuimarika.” Alisema Bw. Marwa
Alisema kuwa tayari kilomita 21 zimefanyiwa kazi mkoani Arusha kwa hatua za awali kwa kuwa kazi hii hufanyika kwa mpangilio wa timu zilizoundwa kitaalam hadi kufikia uwekaji wa alama za mpaka.
Kazi ya uimarishaji wa mpaka kati ya Tanzania na Kenya inayolenga kuwezesha Serikali   kusimamia kwa ufanisi shughuli za mipakani, rasilimali za nchi pamoja na ulinzi na usalama  ilianza katikati ya Mwezi Machi mwaka huu ambapo Kilomita 238 zinaimarishwa kutoka kando ya Ziwa Victoria mkoani Mara hadi Ziwa Natron mkoani Arusha.  

WANAKIJIJI WAUFUKIA MWILI WA MWANAUME ALIYEUA,WADAI WALICHOSHWA NA MATENDO YAKE YA UJAMBAZI

Wananchi wa kijiji cha Isalalo wilayani Nzega wakichimba shimo kwa ajili kuufukia mwili wa Mwanaume mmoja aliyefahamika kwa jina Mijile Peter Nsimbila ambaye anadaiwa kuuawa na watu wasiojulikana baada ya kukatwa mapanga na kisha kuchinjwa na kitu chenye ncha kali akiwa hatua chache kutoka nyumbani kwake.Wananchi hao waliamua kufukia mwili huo wa marehemu Nsimbila pasipo kumpa heshima ya kumzika kwenye kaburi kama ilivyo kwa binadamu wengine hali inayodaiwa imetokana na kuchoshwa na matukio ya uhalifu wa kupindukia aliokuwa akiufanya.
Baadhi ya wananchi wa Kijiji cha Isalalo wakiwa pembeni wakipisha vyombo vya usalama kufanya uchunguzi wa mauaji ya mwanaume mmoja Mijile Peter Nsimbila anayedaiwa kuuawa na watu wasiojulikana ambao walifika kuvamia nyumbani kwake majira ya usiku wakati akijiandaa kulala,Watu hao ambao idadi  haijafahamika  walimkimbiza hatua chache kutoka nyumbani  kwake ndipo walianza kumshambulia kwa silaha za aina mbalimbali hadi kufikia umauti.
Kamanda wa Polisi  mkoa wa Tabora SACP Wilbroad Mutafungwa amethibitisha tukio hilo la mauaji huku akieleza uchunguzi  uliofanywa na Polisi umebaini kuwa marehemu Nsimbila alikuwa akijihusisha na matukio ya ujambazi wa kutumia silaha na kwamba Polisi bado walikuwa wakimsaka kwa udi na uvumba hadi amefikwa na tukio hilo la mauaji.Kumbuku zinaonesha hivi karibuni Marehemu Nsimbila alihukumiwa kutumikia kifungo cha miaka thelathini  baada ya kupatikana na hatia ya kufanya tukio la unyang'anyi wa kutumia silaha na kupora Pikipiki lakini alikata rufaa na kufanikiwa kuachiwa huru.



Tuesday, March 13, 2018

NAIBU WAZIRI MADINI ATEKELEZA AGIZO LA RAIS MAGUFULI, AKIRI CHANGAMOTO ULIPAJI WA FIDIA KWA WANANCHI KUPISHA MRADI WA UCHIMBAJI MADINI

Naibu waziri wa madini Mhe Doto Mashaka Biteko (Mb) akisisitiza jambo wakati akizungumza na wananchi waliojitokeza kwenye mkutano wa hadhara katika Kitongoji cha Mahiga, Kijiji na Kata ya Mwakitoliyo, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli kusikiliza kero za wananchi hao, Juzi 11 Machi 2018. Picha Zote Na Mathias Canal-Wazo Huru Blog
Wakazi wa Kitongoji cha Mahiga, Kijiji na Kata ya Mwakitoliyo, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga wakimsikiliza Naibu waziri wa madini Mhe Doto Mashaka Biteko (Mb) wakati wa mkutano wa hadhara, Juzi 11 Machi 2018.
Mbunge wa Jimbo la Solwa Mhe Ahmed Salum akizungumza na wananchi wa Jimbo hilo kabla ya kumaribisha Naibu waziri wa madini Mhe Doto Mashaka Biteko (Mb) kusikiliza kero za wananchi kwenye mkutano wa hadhara katika Kitongoji cha Mahiga, Kijiji na Kata ya Mwakitoliyo, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Juzi 11 Machi 2018.
Naibu waziri wa madini Mhe Doto Mashaka Biteko (Mb) akiwatuliza wananchi wakati akizungumza kwenye mkutano wa hadhara katika Kitongoji cha Mahiga, Kijiji na Kata ya Mwakitoliyo, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ili kusikiliza mgogoro baina ya wananchi hao na kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering co ltd kutoka nchini China, Juzi 11 Machi 2018
Naibu waziri wa madini Mhe Doto Mashaka Biteko (Mb) (Kushoto) akisikiliza malalamiko kwa baadhi ya Wakazi wa Kitongoji cha Mahiga, Kijiji na Kata ya Mwakitoliyo, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kabla ya mkutano wa hadhara uliofanyika Juzi 11 Machi 2018.

Na Mathias Canal, Shinyanga

Serikali imekiri kuwepo kwa changamoto katika ulipaji wa fidia kwa wananchi waliofanyiwa uthamini katika maeneo yao ili kupisha mradi wa uchimbaji wa madini ya dhahabu kupitia kampuni ya Henan Afro-Asia Geo Engineering co ltd kutoka nchini China.

Akizungumza Juzi 11 Machi 2018 na wananchi waliojitokeza kwenye mkutano wa hadhara katika Kitongoji cha Mahiga, Kijiji na Kata ya Mwakitoliyo, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Naibu Waziri wa wizara ya madini Mhe Doto Mashaka Biteko (Mb) amekiri kuwa zipo changamoto katika jambo hilo hivyo serikali itapitia upya tathimini sambamba na ulipaji wa fidia ili kuhuisha sintofahamu hiyo iliyopelekea wananchi hao kupaza sauti zao za malalamiko.

Mhe Biteko alisema kuwa katika sekta ya madini mnufaika wa kwanza lazima awe mtanzania kwani sheria ya madini ya mwaka 2010 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2017 inaelekeza kuwa na uchumi fungamanishi kwa wananchi ili kuinua pato la wananchi sambamba na mchango wa sekta ya madini kwenye Pato la Taifa.

Aidha, Mhe Biteko aliwasihi wananchi hao kuwa watulivu katika kipindi kifupi ambacho serikali inapitia upya tathmini hiyo huku akiwasihi kuacha uvamizi katika eneo hilo kwani kufanya hivyo ni uvunjifu wa sheria, kanuni na taratibu za nchi.

“Ndugu zangu wananchi Sio kweli kwamba wawekezaji ni wabaya lakini wanapaswa kutambua tu wakija kuwekeza nchini wanapaswa kufuata sheria, kanuni na taratibu za nchi ikiwa ni pamoja na kuwa na mahusiano mazuri na wananchi wanaoishi karibu na mradi huo” Alikaririwa Biteko (Mb)

Machi 10, 2018 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli akihutubia mamia ya wananchi katika eneo la Nyasubi katika Halmashauri ya mji wa Kahama Mkoa wa Shinyanga wakati wa dhifa ya uzinduzi wa barabara ya Isaka-Ushirombo yenye urefu wa Kilomita 132, alimuagiza Naibu Waziri wa wizara ya madini Mhe Doto Mashaka Biteko (Mb) kushirikiana na Mbunge wa Jimbo la Solwa Mhe Ahmed Salum kufanya ziara na kuwasikiliza wananchi kuhusu malalamiko hayo ili serikali kutafuta ufumbuzi wa haraka.

Wananchi hao wanalalamikia kufanyiwa tathmini tofauti na matakwa ya sheria huku wakipatiwa malipo kiduchu pasina kufanyika mkutano wa hadhara wa maridhiano baina ya wananchi na muwekezaji huhu wakiomba kufanyika upya tathmini ya maeneo yao.


Monday, March 12, 2018

ECO BANK TANZANIA KUFADHILI WANAFUNZI SHULE ZA SERIKALI


Ecobank nchini Tanzania kuanzia mwaka huu inaanzisha mpango wa kutoa zawadi ya ufadhili kwa wasichana wanaofanya vyema katika masomo yao kwenye shule za serikali.

Aidha pamoja na ufadhili huo ili kuwaweka katika hali ya kuwa na uzoefu na kazi zao wanazosomea, watakuwa wanahakikisha wakati wa likizo wanawafanyia mpango wa kujishughulisha na kazi hizo ili kuwa na uzoefu.

Hayo yamesema na Mkurugenzi Mkuu benki hiyo nchini Mwanahiba Mzee wakati wa hafla ya mchapalo iliyofanyika hoteli ya Serena kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani mwishoni mwa wiki.

Alisema taasisi yake inaona umuhimu wa kumwezesha mtoto wa kike kusonga mbele kama moto wa taasisi hiyo ya kifedha unavyosema ‘press for progress’ ikimaananisha kujikita katika kutafuta maendeleo.

Alisema mwanamke anafanyakazi nyingi hivyo ni vyema kumwandaa tangu mapema ili kujua majukumu yake kama mzalishaji mkuu kwenye familia.

Alisema kwa sasa hawajaamua wanaanzia ngazi gani za ufadhili, lakini wanataka kufanya kitu tofauti chenye kulenga kupromoti maendeleo ya mtoto wa kike kama maazimio ya Beijing yanavyotaka kufikia asilimia hamsini kwa hamsini katika ngazi za kiutendaji.

Alisema sherehe hiyo ambayo inaambatana na siku ya mwanamke duniani inasherehekewa katika nchi 33 zenye benki hiyo ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kibenki wa kuhakikisha kwamba wanawake wanasonga mbele kwa kuwa idadi yao ni asilimia 49.55 ya watu waliopo duniani na wanahaki ya kusaidia kukua kwa uchumi wa dunia, wa kaya na wakwao wenyewe kwa kuwezeshwa.

Anasema pamoja na ukweli kuwa wanawake wameachwa nyuma kwa miaka mingi, taasisi hiyo imejipanga kuhakikisha kwamba inakuwa na asilimia 50 kwa 50 ifikapo mwaka 2030 huku hapa nchini inakaribia asilimia 49.

Alisema wakati sherehe hiyo ni kusherehekea mafanikio na kujifunza kutoka kwa wanawake waliofanya vyema, wanawake wanatakiwa kujiuliza wamesaidiaje wanawake wenzao kufikia ngazi ya juu kabisa ya uwezo walionao.

Alisema katika taasisi yake wametengeneza mpango wenye vipengele vitano vya kuhakikisha kwamba suala la jinsia linazingatiwa. Alitaja vipengele hivyo kama kushawishi fikira za jinsia katika maeneo ya kazi kuona kwamba kuna mizania. 

Kukabili fikira mgando dhidi ya wanawake, kuwezesha mwanamke kuonekana wazi, kushawishi kuinua wanawake kwa kutwaa huduma bora wanazozitoa na kusherehekea mafanikio ya mwanamke.

Alisema amefurahishwa na jinsi wanawake majasiri kama Getrude Mongella walivyoweza kupigania haki za wanawake wakikabiliana na makandokando yake na kufanikisha maazimio ya Beijing ambayo yanatumika kumkomboa mwanamke.

Hata hivyo, Mkurugenzi huyo alisema pamoja na kupokea maelekezo ya mama Mongella kuhusu ustawishaji wa mwanamke, aliwataka wanawake kuwa wajasiri na kupambana na hali zao bila kujali wanatoka katika mazingira gani.

Alisema yeye alisoma katika shule ambazo sasa zinaitwa za Kayumba (shule za Upe) akianzia Mizumbwini Kibada hadi Kurasini kabla ya kupata nafsi ya kusoma Masjid Quba iliyopo Sinza na Alharamain alipomalizia kidato cha sita.

Unaona nimesoma shule za kawaida tu, siri kubwa ni kujituma na kujitambua. Nilijituma kwani niliona familia ya mama yangu ni watu maskini japo familia ya baba yangu walikuwa wanajiweza, nilisema lazima nimsaidie mama yangu.

Mwanahiba alisisitiza katika mazungumzo yake kwamba kujituma kunasaidia sana kwani hata yeye alipo ajiriwa kwa mara ya kwanza kama karani na kulipwa sh laki moja hakujali kwani alijua ni nafasi yake ya kujifunza japo alikuwa na MBA.

Aidha alisema kwamba alijifunza kwa bidii na kujenga kuaminika wakati akiwa Stanbic hali iliyompatia heshima ya jina lake kupelekwa katika mamlaka za Benki ambako alipita michujo mbalimbali na kufanikiwa kupata nafasi ya Ukurugenzi Mkuu Ecobank.

Naye Mama Mongella, mwanasiasa mkongwe nchini na mpigania haki za wanawake aliyeshiriki Mkutano wa Beijing, akitoa nasaha zake, alimtaka Mkurugenzi wa Ecobank kuwapatia wanawake mitaji ili waweze kumiliki viwanda vyao waweze kuajiri na kufukuza.

Aidha aliwataka wafanyakazi wa benki hiyo kutomwangusha mkurugenzi wao na kuhakikisha wanajituma zaidi hasa benki inapowania kuwa na asilimia 50 kwa 50 katika utendaji wake.

Alisema wakati taifa hili linaelekea katika viwanda benki hiyo inayoendeshwa na mwanamama inastahili kupigania maslahi ya wanawake ili wawe na viwanda na kuchangia katika uchumi badala ya wao kuwa wasindikizaji.

"Si kuwakorogea uji wanaofanya viwandani bali wao ndio wawe wenye restaurants (migahawa) … wenye viwanda.." alisema mama Mongella.

Aidha aliwataka wanawake wanapopata nafasi ya kuajiriwa wawe makini katika utumishi wao na kuacha kuwataka mabosi ndio wawapigie magoti.

Pamoja na kutaka wanawake waendelezwe aliitaka jamii isisahau watoto wakiume kwani nao wanastahili kupata haki za elimu ili waweze kuwa watu bora na wanaoelewa.

Kama sasa kuna matatizo je kama wasipoenda shule wakabaki kuwa wapumbavu matatizo si yatazidi zaidi, alihoji mama Mongella.

Alkiwataka wanawake katika kila nafasi yao kufanya vyema na kuaminika huku wakiwasaidia wanawake wenzao kusonga mbele ili waweze kuwa na chakula cha kutosha kuwawezesha kufanya maamuzi yaliyoshiba pia.

Akizungumzia tasnia ya habari alisema kwamba toka walipotoka katika mkutano wa Beijing waandishi wa habari wamekuwa ndio wenye mabadiliko makubwa wakiwabeba wanawake katika muonekano mzuri na kumshauri Mkurugenzi huyo kuwatumia waandishi kuonesha watu mambo makubwa yanayofanywa na wanawake.

Alisema yeye na mafanikio aliyonayo sasa ni matokeo ya uamuzi wa kutaka kukabiliana na matatizo ya kiuchumi ambapo aliona jinsi mwanamke wa kijijini anavyohangaika na kusema ataendelea kupigana kumbadilisha mwanamke awe katika maisha bora.

Alisema amebahatika kuwa na watoto watatu wote wanaume, lakini amesema mabinti watakaoingia katika mji wake atahakikisha kwamba anawahoji wamefanya nini au wanampango gani wa kusaidia wanawake wenzao.

Katika hafla hiyo ya mchapalo wanawake walibadilishana mawazo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuwa na wakati wa kujifunza na kushangilia mafanikio ya mwanamke.
Mshehereshaji Babbie Kabae (kulia) akitambulisha wageni waalikwa kwenye hafla mchapalo ya kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani iliyoandaliwa na Ecobank Tanzania na kufanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Mjasiriamali mwenye uthubutu ambaye pia ni mteja wa Ecobank Tanzania, Halima Mamuya akijitambulisha na ku-“share” uzoefu wake katika ujasiriamali wakati wa hafla mchapalo ya kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani iliyoandaliwa na Ecobank Tanzania na kufanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Kutoka kushoto ni Ofisa Uchumi na Mipango wa jiji la Mwanza, Bertiller Masawe, Mjasiriamali Chance Bishikwabo, Mgeni rasmi Mwanasiasa Mkongwe nchini na mpigania haki za wanawake, Mama Getrude Mongella pamoja na Mkurugenzi Mkuu Ecobank Tanzania, Mwanahiba Mzee wakisikiliza kwa umakini shuhuda za Mama Mamuya.</ p>
Mkurugenzi Mkuu Ecobank Tanzania, Mwanahiba Mzee akizungumza kabla ya mgeni rasmi ambapo alielezea kwa undani safari ya maisha kama mwanamke wakati hafla mchapalo ya kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani iliyoandaliwa na Ecobank Tanzania na kufanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Mgeni rasmi Mwanasiasa Mkongwe nchini na mpigania haki za wanawake, Mama Getrude Mongella akitoa nasaha zake kwa wageni waalikwa na wafanyakazi wa Ecobank Tanzania (hawapo pichani) wakati wa hafla mchapalo ya kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani iliyoandaliwa na Ecobank Tanzania na kufanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Mchungaji Basilisa Ndonde akielezea kuhusu nafasi ya mwanamke katika familia na majukumu yake kama mke wakati wa hafla mchapalo ya kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani iliyoandaliwa na Ecobank Tanzania na kufanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Mgeni rasmi mwanasiasa mkongwe nchini na mpigania haki za wanawake, Mama Getrude Mongella akipiga selfie na baadhi ya wageni waalikwa wakati wa hafla mchapalo ya kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani iliyoandaliwa na Ecobank Tanzania na kufanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Mgeni rasmi mwanasiasa mkongwe nchini na mpigania haki za wanawake, Mama Getrude Mongella katika picha ya pamoja na baadhi ya wageni waalikwa wakati wa hafla mchapalo ya kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani iliyoandaliwa na Ecobank Tanzania na kufanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Kushoto ni Mkuu wa Kitengo cha Miamala Ecobank Tanzania, Wende Mengele.< /p>
Mkuu wa kitengo cha Masoko na Mawasiliano Ecobank Tanzania, Furaha Samalu (kulia) katika picha ya pamoja na baadhi ya wageni waalikwa wakati wa hafla mchapalo ya kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani iliyoandaliwa na Ecobank Tanzania na kufanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.
Baadhi ya wageni waalikwa katika picha ya pamoja wakati wa hafla mchapalo ya kusherehekea mafanikio ya mwanamke katika Siku ya Wanawake duniani iliyoandaliwa na Ecobank Tanzania na kufanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.

Saturday, March 10, 2018

EXCLUSIVE INTERVIEW – FAHAMU CHIMBUKO LA MATIMILA BENDI, NA MIKAKATI ILIYOPO KWA SASA

Kushoto ni Mtangazaji wa Ruvuma TV Nancy Mbogoro akimuuliza swali Mpenda Mvula ambaye ni mtoto wa marehemu Abrose Mvula aliyekuwa mmiliki wa bendi ya Super Matimila.
..................................
Mtoto wa Mzee Abrose Mvula ambaye ndiye alikuwa mmiliki wa bendi ya Super Matimila aelezea chimbuko la  bendi hiyo , Historia ya bendi,kwa nini iliitwa matimila,ilikuwaje mzee wake akaanzisha bendi hiyo pamoja na historia  ya Remmy Ongala akiwa na bendi ya Matimila na mikakati iliyopo juu ya bandi hiyo kwa sasa.

Thursday, March 8, 2018

MBUNGE VITIMAALUM MUNDE TAMBWE AMEWASAIDIA WANAWAKE MIAMOJA KADI ZA MATIBABU NA MIFUKO MIAMBILI YA SARUJI KWA AJILI YA UJENZI MABWENI,ZAHANATI

Mbunge wa Vitimaalum mkoa wa Tabora Munde Tambwe akizungumza katika Sherehe za Maadhimisho ya Siku ya Wanawake zilizofanyika kimkoa mkoani Tabora,katika maadhimisho hayo Munde aliwalipia  Kadi za matibabu maarufu TIKA Wanawake wasio na uwezo Miamoja wanaoishi manispaa ya Tabora akiwa anakamilisha idadi kama hiyo kwa Wanawake wengine mia moja kwa kila Wilaya za mkoa wa Tabora ambazo ni wilaya saba.
Munde akikabidhi jumla ya shilingi milioni moja kwa Mke wa Rais mstaafu wa awamu ya nne Mama Salma Kikwete kwa ajili ya kulipia Kadi hizo miamoja za matibabu kwa Wanawake wasio na uwezo wa kumudu gharama za matibabu Manispaa ya Tabora.
Mke wa Rais Mstaafu Mama Salma Kikwete akimpongeza Mbunge wa Vitimaalum mkoa wa Tabora Munde Tambwe baada ya kupokea kiasi cha shilingi milioni moja kwaajili ya TIKA huku Mbunge huyo Munde Tambwe akiahidi mbele Mama Salma Kikwete kuchangia jumla ya mifuko Miambili   ya Saruji kwa ajili ya Ujenzi wa Mabweni katika Shule za Sekondari za kata manispaa ya Tabora na ujenzi wa uzio Kliniki ya Tabora mjini maarufu Town Clinic.

Mke wa Rais mstaafu wa awamu ya nne Mama Salma Kikwete akizungumza katika maadhimisho hayo ambapo  alisema kuna haja ya kuleta mabadiliko ya kisekta yatakayoharakisha   maendeleo kwa Wanawake kupitia kujenga misingi imara ya kupata elimu bora itakayotoa fursa  kwa  Wanawake  kuajiriwa na hata kujiajiri wenyewe.
Maadhimisho  ya Siku ya wanawake duniani mkoani Tabora ambapo Mama Salma Kikwete alikuwa mgeni rasmi iliyofanyika viwanja vya Chipukizi mjini Tabora.
Mkuu  wa mkoa wa Tabora  Aggrey Mwanry akiungana na Wanawake mkoani Tabora kuadhimisha siku hiyo ya Wanawake duniani
Gwiji na Msanii mkongwe wa muziki wa Taarabu nchini Malkia Khadija Kopa akitumbuiza katika maadhimisho hayo mjini Tabora katika viwanja vya Chipukizi.
Wanawake wajasiliamali wakiadhimisha siku yao wakati muziiki wa taarabu ukitumbuizwa na Malkia Khadija Kopa.






Tuesday, December 12, 2017

TIGO YAZINDUA DUKA LA KISASA URAMBO IKIWA NI MUENDELEZO WA KUBORESHA HUDUMA KWA WATEJA WAKE

Mgeni rasmi  Katibu Tawala Wilaya  ya Urambo  Bw.Paschal  Byemelwa  akikata  utepe  ikiwa  ni  Uzinduzi wa Duka la Kisasa la Kampuni ya Simu za kiganjani ya Tigo wilayani Urambo katika kutekeleza adhma ya kusogeza karibu huduma za mawasiliano kwa wananchi wilayani humo,Kutoka kulia ni Mkurugenzi mtendaji halmashauri ya wilaya ya Urambo Bi.Margareth Nakainga,wapili kulia ni Meneja wa Tigo kanda ya Ziwa Bw.Gwamaka Mwakilembe,na wa kwanza kushoto ni Meneja wa Tigo mkoa wa Tabora  Bw.Bright Kisanga.

Duka la kisasa la Huduma kwa Wateja wa Tigo Wilayani Urambo

Mgeni Rasmi  Paschal  Byemelwa,kulia ni Mkurugenzi mtendaji halmashauri ya wilaya ya Urambo Bi.Margareth Nakainga,wapili kutoka  kulia ni Meneja wa Tigo kanda ya Ziwa Bw.Gwamaka Mwakilembe,na wa kwanza kushoto ni Meneja wa Tigo mkoa wa Tabora  Bw.Bright Kisanga wakipiga makofi kushangilia tukio la kutaka utepe kama ishara ya Uzinduzi wa Duka hilo la Kisasa wilayani Urambo.

Picha ya pamoja baada ya Uzinduzi wa Duka hilo
Mmoja kati ya maafisa wa Tigo  Bi.Tunu Kazinja  akitoa maelezo kwa huduma ambazo wanazitoa mara baada ya uzinduzi wa Duka hilo la Kisasa wilayani Urambo.

Mgeni Rasmi  Katibu Tawala wilaya ya Urambo Paschal Byemelwa pamoja na wageni wengine waalikwa katika hafla fupi ya uzinduzi wa Duka hilo la kisasa,walipata fursa ya kuangalia bidhaa mbalimbali za Tigo ambazo zilikuwa zikioneshwa nje ya Duka hilo la Kisasa.
Baadhi ya wananchi wa wilaya ya Urambo wakipata maelezo ya huduma zinazotolewa na Kampuni ya Tigo katika moja ya Banda la maonesho wakati wa hafla fupi ya Uzinduzi wa duka la Kisasa wilayani Urambo.

Katibu Tawala wilaya ya Urambo Bw.Paschal Byemelwa akihutubia wakati wa Uzinduzi wa duka la Tigo  wilayani Urambo ambapo ameishukuru kampuni ya Tigo kwa kufungua Duka hilo la Kisasa ambalo amesema litasaidia kuwapunguzia adha kubwa wananchi wa Urambo ambao walikuwa wanalazimika kusafiri umbali mrefu kufuata huduma. 
Baadhi ya wananchi wa Urambo wakimsikiliza katibu tawala wilaya ya Urambo Bw.Paschal Byemelwa wakati akiwahutubia katika hafla fupi ya uzinduzi wa duka hilo la kisasa.
Meneja wa kanda ya ziwa wa Tigo Bw.Gwamaka Mwakilembe akizungumza na wananchi wa Urambo wakati wa uzinduzi wa Duka la kisasa wilayani humo ambapo alieleza kuwa kampuni ya Tigo  ambayo inaongoza kwa mageuzi ya kidigital nchini imeamua kuzindua duka hilo ikiwa ni muendelezo wa juhudi zake kuboresha huduma kwa wateja wake.




Monday, October 2, 2017

MAHAKAMA YAAMURU MSHITAKIWA HARBINDER SETHI AKATIBIWE HOSPITALI YA TAIFA YA MUHIMBILI NDANI YA SIKU 14

Harbinder Sethi

Na Dotto Mwaibale

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imeamuru kwa mara nyingine mshtakiwa Harbinder Sethi akatibiwe katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ndani ya siku 14.

Korti imesema iwapo hilo halitatekelezwa, mkuu wa gereza afike mahakamani kujieleza. Sethi yupo mahabusu katika Gereza la Segerea.

Saturday, June 24, 2017

SHUJAAZ WAWAFUNDA WAANDAAJI WA MASHINDANO YA EAST AFRICA CUP 2017

Mkuu wa utafiti wa Kampuni ya Well Told Story,Dkt Anastasia Mirzoyants akitoa maelezo kwa washiriki wa Warsha iliyoandaliwa na  Mradi wa Shujaaz  iliyofanyika Hotel ya Uhuru mjini Moshi.
Baadhi ya Washiriki wa Warsha iliyoandaliwa na watayarishaji wa Mradi wa Shujaaz kwa ajili ya kutoa eimu juu ya maswala mbalimbali ikiwemo Ujasiliamali pamoja na Kilimo,Warsha ambayo inafanyika sambamba na Mashindano ya Kimataifa ya Vijana kwa vijana wa nchi za Afrika Mashariki.
Mkuu wa utafiti wa Kampuni ya Well Told Story,Dkt Anastasia Mirzoyants akitoa maelezo kwa washiriki wa Warsha iliyoandaliwa na  Mradi wa Shujaaz  iliyofanyika Hotel ya Uhuru mjini Moshi
Washiriki katika Warsha hiyo.
Mkuu wa utafiti wa Kampuni ya Well Told Story,Dkt Anastasia Mirzoyants akizungumza na Wanahabari mara baada ya kumalizika kwa Warsha iliyoandaliwa na  Mradi wa Shujaaz  iliyofanyika Hotel ya Uhuru mjini Moshi
Baadhi ya Vijana waliofanikiwa kuingia katika Kijiji cha Shujaaz wakionesha umahiri wao katika uimbaji ambapo pia walipata zawadi kutoka Shujaaz.
Timu za watoto chini ya miaka 13 za Msimamo na Right to Play kutoka Dar es Salaam zikichuana katika mashindano ya East Africa Cup 2017 yanayofanyika katika viwanja vya shule ya sekondari ya Moshi Ufundi.
Vijana chini ya miaka 13 wakioneshana umahiri  katika kusakata soka katika mashindano ya East Africa Cup 2017 yanayofanyika katika viwanja vya Moshi Technical.
Baadhi ya vijana wakifuatilia mchezo huo.
Katika Kijiji cha Shujaaz wakishiriki michezo mbalimbali ikiwemo ya kukimbia huku wakiwa ndani ya magunia.
Kijiji cha Shujaaz kimekuwa kivutio kikubwa kwa vijana wanaoshiriki mashindano ya East Africa Cup 2017.

Na D ixon Busagaga wa Globu ya Jamii ,Kanda ya Kaskazini.