Pages

KAPIPI TV

Thursday, January 19, 2017

SEMINA YA KUPEANA TAARIFA KUHUSU UTOAJI MIMBA USIO SALAMA

1
Mkurugenzi Mtendaji wa Chama Cha wanasheria wanawake TAWLA Bi Tike Mwambipile akifungua semina ya kuhamasisha wadau wa Kutetea haki za wanawake na kujadili madhara ya utoaji mimba usio salama hapa Tanzania kwa kushirikishana matokeo ya utafiti uliofanyika hivi karibuni wa matukio ya utoaji mimba usio salama pamoja na huduma za baada ya utoaji mimba usio salama hapa Tanzania.
2
Baadhi ya washiriki wa semina hiyo wakifuatilia mada kadhaa zilizokuwa zikitolewa katika semina hiyo.
3
Dk. Pensiens Mapunda Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Afya na Tiba Hurbert Kairuki HKMU akielezea jambo wakati wa semina hiyo.
4
Baadhi ya washiriki wakisikiliza kwa makini mambo mbalimbali yaliyokuwa yakijadiliwa katika semina hiyo.
7
5
Washiriki wa semina hiyo wakiwa katika picha ya pamoja.
...........................................................................
Lengo la semina hii ni kujadili swala nyeti linaloigusa jamii yetu ya Kitanzania na wadau muhimu katika kutetea haki za wanawake katika kuhakikisha ustawi wa mwanamke unaendelea vizuri katika jamii yetu
Pamoja na kazi tunazofanya za kutoa huduma ya msaada na ushauri wa kisheria kwa wanawake na watoto, TAWLA imejikita pia katika kupigania haki za wanawake na usawa wa kijinsia hapa nchini ikiwemo Haki ya Afya ya Uzazi. Hii ni kwa sababu, TAWLA inatambua umuhimu wa haki za kijinsia na Afya ya Uzazi katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii na zaidi sana kuondoa imani potofu kuhusu afya ya uzazi.
TAWLA kupitia vituo vyake vya msaada wa kisheria na mijadala ya kijamii (Community Conversation) tulipata taarifa za madhara na vifo vitokanavyo na utoaji mimba usio salama ambazo zilitushtusha na kutugusa sana na ndio maana tukaonelea kuwa ni vyema takafanya utafiti juu ya suala hili ili kuona ni kwa namna gani tunaweza kuisaidia jamii yetu kwa kushirikiana na wadau muhimu katika swala hili, ili kupunguza au kuondoa kabisa vifo vya akina mama na wasichana vitokanavyo na utoaji mimba usio salama.
Takwimu za tafiti ya Guttmacher zinaonyesha kwamba utoaji mimba usio salama ni sababu ya pili ya vifo vya akina mama na wasichana hapa nchini kwa maana kwamba:
(1) Kila mwaka wanawake wa Kitanzania 405,000 hutoa mimba kwa usiri karibu wote na kwamba 40% hupata matatizo ambayo yanahitaji matibabu:
(2) Kila mwaka wanawake wa Kitanzania milioni moja hupata mimba zisizotarajiwa ambazo 39% ya wanawake hao huishia kwenye utoaji mimba:
(3) 60% ya wanawake wa Tanzania wenye matatizo ya utoaji mimba hawapati huduma ya matibabu wanayoihitaji:
(4) Kila mwanamke 1 kati ya wanawake 5 nchini Tanzania ana mahitaji yasiyofikiwa ya uzazi wa mpango
Ni kwa misingi hiyo basi kongamano hili lina malengo makuu yafuatayo:
(1) kuhamasisha washiriki na kujadili madhara ya utoaji mimba usio salama hapa Tanzania kwa kushirikishana matokeo ya utafiti uliofanyika hivi karibuni wa matukio ya utoaji mimba usio salama pamoja na huduma za baada ya utoaji mimba usio salama hapa Tanzania:
(2) Kushirikishana matokeo ya utafiti uliofanyika hivi karibuni wa matukio ya utoaji mimba usio salama pamoja na huduma za baada ya utoaji mimba usio salama hapa Tanzania:
(3) Kubadilishana uzoefu:
(4) Kufanya uchechemuzi wa kuingizwa kwenye Sheria za Tanzania vipengele vinavyohusu haki ya Afya ya Uzazi vilivyopo kwenye Mkataba wa Nyongeza wa Afrika (Maputo Protocol) juu ya Haki za Wanawake:
(5) Kuwakutanisha wadau muhimu juu ya swala hili ili kujadili kuhusu Sheria na Sera zinazohusu Haki ya Afya ya Uzazi na utoaji mimba ulio salama hapa Tanzania.
Pamoja na madhumuni yaliyoiainisha hapo juu, semina hii inakusudia kutambua aina ya michango ambayo wadau mbali mbali waliopo hapa leo wanaweza kutoa katika kupunguza vifo vya akina mama vinavyotokana na utoaji mimba usio salama na madhara yake hapa Tanzania
Chama Cha Wanasheria Wanawake Tanzania kinaamini kwamba, kutambua Haki ya Afya ya Uzazi ni muhimu katika kufikia lengo la kupigania haki za wanawake na usawa wa kijinsia hapa nchini.. Lengo hili linaweza kukamilika endapo tu kila mmoja wetu katika ukumbi huu atajitoa katika kuhakikisha kuwa, wototo wetu wa kike, dada zetu, mama zetu na wanawake wote hapa nchini hawafi kwa sababu ya utoaji mimba usio salama.
Tunatambua kazi za Taasisi/ofisi zenu katika kuletea haki za binadamu, haki za wanawake na usawa wa kijinsia hapa Tanzania, ndio maana tumeomba ushiriki wenu ili kufanikisha lengo hili la kuleta haki katika jamii yetu.
Washiriki wa semina hii ni Baadhi ya wadau kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Wizara ya Katiba na Sheria na baadhi ya Asasi zisizo za kiraia zinazoshughulikia maswala ya haki za wanawake Nchini Tanzania.

No comments: