Pages

KAPIPI TV

Wednesday, March 4, 2015

WANANCHI WALALAMIKIA UCHELEWESHWAJI WA UPIMAJI WA ARDHI,WAHOFIA KUPOKONYWA NA WATENDAJI WA HALMASHAURI YA MANISPAA-TABORA


Baadhi ya wakazi wa eneo la Uledi kata ya Ipuli Manispaa ya Tabora wakiwa katika mkutano wa dharura wa kujadili hatma ya kupimiwa ardhi yao ambayo wamepinga kupimiwa na halmashauri ya manispaa ya Tabora kwa madai kwamba ina mpango wa kuwadhurumu kwa kuwapatia fidia ya kiasi cha shilingi laki sita huku wakiitaka kampuni ya Ardhi Plan Limited kuwapimia kwa kuwa itawapatia viwanja miongoni mwa watakavyopimiwa ambavyo wataviuza kwa kiasi cha shilingi milioni moja na kuendelea.
Wananchi wakiangalia michoro ya ramani ya viwanja vyao iliyochorwa na Kampuni ya Ardhi Plan Limited



Na Mwandishi wetu.
Wananchi zaidi ya 1144 eneo la Uledi kata ya Ipuli Manipaa ya Tabora wamelalamikia ucheleweshwaji wa upimaji wa ardhi ya maeneo wanayoishi hatua ambayo imewatia hofu ya kuona kuwa huenda wakaporwa maeneo hayo na baadhi ya watendaji wachache wa kitengo cha ardhi manispaa ya Tabora.

Wakizungumza katika mkutano wa dharura ulioitishwa na kamati ya ardhi iliyoteuliwa na wananchi hao baada ya kubaini kuwa upo uwezekano wa kupoteza maeneo yao kufuatia halmashauri ya manispaa ya Tabora kusuasua kuwapimia  maeneo  yao  ambayo  wanahitaji kuyaendeleza kwa ajili ya makazi,walisema kuwa hawatakuwa tayari kuona wanapoteza haki yao ambayo itaporwa na wajanja wachache.

Mwenyekiti wa kamati ya ardhi ya eneo hilo la Uledi Bw.Aman Mbwambo alisema licha ya kuendelea  kudai  wapimiwe  maeneo yao kwa zaidi ya miaka mitano na hata kufikia hatua ya kufungua kesi mahakamani kitengo cha ardhi mwaka 2012 na mahakama kutoa uamuzi wa kuwapa haki ya kupimiwa lakini halmashauri ya manispaa ya Tabora bado imeshindwa kutekeleza agizo hilo la mahakama.

Mbwambo alisema  baada  ya  kubaini  kuwepo kwa mizengwe inayofanywa na baadhi  ya  watendaji wa  halmashauri  ya  manispaa ya  Tabora kamati yake ilipewa baraka na wakazi wa eneo hilo la Uledi kuingia mkataba na kampuni ya Ardhi Plan Limited kupima viwanja hivyo hatua ambayo pia iliridhiwa na baraza la Madiwani wa  halmashauri ya manispaa ya Tabora.

Kufuatia makubaliano yaliyofikiwa  baina ya wakazi wa Uledi na Kampuni ya Ardhi Plan Limited ya kupima viwanja hivyo ambavyo wananchi hao wanadai kuwa watanufaika kwa kuuza kila kiwanja kimoja kati ya shilingi milioni moja hadi  moja na laki tano kupitia Kampuni hiyo,huku halmashauri ikihitaji kupima yenyewe na kufidia kila kiwanja kwa kulipa wananchi  hao  shilingi  laki sita,jambo ambalo wamedai kuwa ni wizi wa mchana kweupe.

Kwaupande wake Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Ardhi Plan Limited Bw.Gombo Samandito alisema kampuni yake tayari imekwisha yapima maeneo hayo na kuyafanyia uhakiki kwa kila mwananchi ikiwa ni pamoja na kuchora ramani ya viwanja hivyo lakini jambo la kusikitisha ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri ya manispaa ya Tabora imeshindwa kutoa kibali cha kuruhusu taratibu zingine kuendelea ikiwa ni pamoja na kuweka mawe ya msingi na kuanza kuchonga barabara za mitaa kwa kufuata kanuni za mipango miji.

Hata hivyo baadhi ya wananchi katika mkutano huo wa dharura wa kujadili hatma ya kupimiwa maeneo yao,wameonesha kushitushwa kwao na kitendo cha watumishi wa Idara ya ardhi manispaa ya Tabora kuingia kinyemela na kuanza kuwapimia baadhi ya watu na kuwauzia maeneo hayo jambo ambalo limeendelea kuzidisha chuki dhidi ya wananchi hao ambao wameiomba serikali kuingilia kati mgogoro huo.

“Jamani hivi sasa naomba tuanze kupeana taarifa ikiwa mtu atamuona huku mtumishi wa idara ya ardhi anakuja kupima tumkamate na kumuadhibu sisi wenyewe hata kama tutakuwa tumejichukulia sheria mkononi si vibaya kwani tupo tayari kufa kwa ajili ya kudai haki zetu”alisema mmoja wa wananchi katika mkutano huo.

Aidha wananchi hao wamekuwa wakifanya mikutano  ya mara kwa mara kwa lengo la kujadili hatua ya halmashauri kusuasua kuwapimia maeneo yao lakini hadi sasa hakuna taarifa zozote zinazotolewa na ofisi ya Mkurugenzi wa halmashauri ya manispaa ya Tabora kuhusu mgogoro huo uliodumu kwa zaidi ya miaka mitano.
      

No comments: