Pages

KAPIPI TV

Friday, September 19, 2014

MTOTO ALIYEZALIWA BILA SEHEMU YA KUTOLEA HAJA KUBWA AFANYIWA UPASUAJI

Na Allan Ntana, Sikonge

MTOTO Pili Ibrahimu (4) aliyezaliwa mwezi Februari 2010 katika zahanati ya Mole iliyoko katika kijiji cha Mole Kiloleli kata ya Mole wilayani Sikonge mkoani Tabora bila kuwa na sehemu ya kutolea haja kubwa amefanyiwa operesheni na madaktari bingwa katika hospitali ya Rufaa Bugando ili kumwezesha kuwa na kiungo hicho muhimu katika mwili wake.

Binti huyo alifanyiwa upasuaji katika hospitali hiyo wiki mbili zilizopita baada ya wasamaria wema kujitokeza na kutoa michango ya fedha kiasi cha sh mil 2 ili kufanikisha safari ya kumpeleka hospitali ya Rufaa Bugando iliyoko jijini Mwanza kwa ajili ya matibabu kama wazazi wake walivyokuwa wameshauriwa na wataalamu wa afya.

Mafanikio ya safari na matibabu ya mtoto Pili kwa kiasi kikubwa yalichangiwa na moyo wa huruma na jitihada za kipekee zilizofanywa na Meneja wa shirika la Care International wilayani Sikonge Waziri Rashid Njau kwa kushirikiana na Muuguzi wa zahanati ya kijiji hicho Bi.Deodata Raphael Lyimo aliyetoa taarifa za kuwepo kwa mtoto mwenye tatizo hilo.

Baada ya kupata taarifa za Pili, Njau alilazimika kusambaza taarifa za mtoto huyo katika mitandao mbalimbali ya kijamii ili kutafuta msaada toka kwa wasamaria wema jambo ambalo liligusa watu wengi sana ndani na nje ya mkoa wa Tabora na kuanza kutoa michango yao.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya mtoto huyo kurejea kutoka Bugando alikofanyiwa upasuaji, ‘Njau akiwa amejawa na furaha’, alitoa shukrani zake za dhati kwa watu wote walioguswa na tatizo la mtoto huyo na kutoa msaada uliowezesha kupelekwa Bugado kwa ajili ya upasuaji zoezi lililofanyika kwa mafanikio makubwa.
 
Njau alibainisha kuwa Pili alikuwa anateseka sana kwa sababu haja kubwa ilikuwa inatokea sehemu ya haja ndogo na kupata maumivu makali sana kila wakati kwa kipindi chote hicho cha miaka minne jambo lililomfanya akimbiwe na watoto wenzake na kubaki mpweke.

Akizungumzia tatizo hilo mama mzazi wa Pili, Hamisa Masudi (35) alisema hali ya mwanae ilishamkatisha tamaa hasa ukizingatia kuwa anaishi maisha ya umaskini sana na hakuwa na uwezo wowote wa kumpeleka kwenye hospitali kubwa na mbaya zaidi mume wake alishamkimbia baada ya kuona amejifungua mtoto mwenye ulemavu.

Naye Deodata Raphael Lyimo muuguzi wa zahanati ya Mole alipongeza jitihada zilizofanywa na shirika la Care International kupitia mradi wake wa TABASAMU ambazo zimefanikisha matibabu ya mtoto huyo na sasa anaendelea vizuri huku akibainisha kuwa msaada zaidi bado unahitajika kwa vile mtoto huyo anatakiwa kupelekwa tena Bugando mwezi ujao kwa ajili ya uchunguzi wa maendeleo ya upasuaji uliofanyika.

Aidha alimshukuru Meneja wa Care International wilayani Sikonge kwa utayari wake na moyo wa kujali kwani baada ya kupewa taarifa za kuwepo kwa mtoto mwenye tatizo hilo kijijini hapo wakiwa katika ziara ya kukagua huduma za afya ya uzazi kwa wajawazito katika vituo vya afya na zahanati aliagiza mtoto huyo aletwe mara moja amwone.

No comments: